Wednesday, December 31, 2014

CCM KUTUMIA PANGA LA 2005

 
Vigezo 13 vilivyowekwa na CCM katika Uchaguzi Mkuu wa 2005 kumpima mwanachama anayefaa kugombea urais, ndivyo vitakavyotumika kuwaengua makada wanaoendelea kujitokeza kuwania nafasi hiyo mwakani, imefahamika.
Vigezo hivyo vinaonekana kuwa kizingiti kwa baadhi ya makada wa chama hicho ambao tayari wametangaza na wengine wanaotajwa kutaka nafasi hiyo ya juu nchini, ukiachilia mbali mnyukano unaotarajiwa kutoka vyama vya upinzani vinavyoonekana kupata nguvu.
Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Philip Mangula amelithibitishia gazeti hili kwamba, “Sifa hizo 13 zilizotumika mwaka 2005 na 2010 ndizo zitakazotumika pia mwaka 2015 na wala hakutakuwa na maboresho wala nyongeza ya aina yoyote.”
Asante kwa kutembelea blog hii ya Jambo Tz, ili kuboresha blog yetu tunatoa fulsa ya kutangaza matangazo mbalimbali na pia kutoa maoni yako kupitia namba ya simu (WhatsApp & SMS) 0715 221198, E-mail jambotz8@gmail.com. Merry Chistmass & Happy New Year.
Vigezo hivyo viliwekwa ili kuhakikisha chama hicho kinampata mgombea asiyetiliwa shaka juu ya vitendo vya uadilifu, mwenye uzoefu wa uongozi serikalini, atakayedumisha muungano, mwenye upeo wa masuala ya kimataifa, mtetezi wa wanyonge, asiyejilimbikizia mali na mwajibikaji, mambo ambayo hata hivyo, bado yameibua mjadala iwapo yanazingatiwa au la.
Pia anayetakiwa lazima awe mwenye kuzitetea sera za CCM, anayekubalika na wananchi, asiye na hulka ya udikteta au ufashisti, mwenye uwezo wa kufanya uamuzi wa busara na kiwango cha elimu ya chuo kikuu au inayolingana nayo.
Licha ya vigezo hivyo, baadhi ya makada waliokwishajitokeza na wengine wanaotajwa wanaonekana dhahiri kukosa baadhi sifa hizo na wengine wako ‘kifungoni’ kwa miezi 12 baada ya kupewa onyo kali kwa kufanya kampeni mapema na kujihusisha na vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya chama na jamii.
Vigogo wa CCM ambao wanatajwa kutaka kupewa ridhaa ya kupeperusha bendera ya chama hicho ambao iwapo watachukua fomu, watatazamwa kwa vigezo hivyo ni Mbunge wa Nzega, Dk Khamis Kigwangalla, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba ambao wamekwishatangaza kuwania nafasi hiyo.
Wengine ambao wanatajwa ingawa hawajatangaza nia hadharani ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa; Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa; Bernard Membe; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu); Stephen Wasira na aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja.
Wachambuzi wanavyosema
Akizungumzia vigezo hivyo, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Tumaini, Danford Kitwana alisema CCM inajua kuwa hakuna mgombea anayeweza kuwa na sifa zote 13, kwa hiyo inapaswa iangalie ni nani anawazidi wengine.
“Kigezo cha kuwa na sifa ya maadili ndicho kinachowakwamisha wengi, pia hakuna mgombea anayeweza kuwa na sifa zote zilizowekwa na chama, mwingine anaweza kuwa na sifa saba, nne au tano.
“Wakitumia mfumo wa kuwatazama wagombea wao kwa idadi ya sifa, mtu mwenye sifa nyingi ndiye asimamishwe kugombea.”
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria Tanzania (OUT), Dk Emmanuel Mallya alisema Tanzania inahitaji kuongozwa na rais mwenye historia ya uadilifu wa matumizi ya fedha za umma.
“Tunahitaji kiongozi anayeweza kusimamia fedha za umma, si mtu anayenunua vitu ovyo bila kujali Hazina kuna kiasi gani, hilo ni tatizo kubwa,” alisema Dk Mallya.
Aliongeza kuwa, kiongozi huyo lazima awe mchapakazi anayeweza kuwaletea wananchi maendeleo, lakini watu wengi wamekuwa wakisema wanamtaka mtu mwadilifu bila kuzungumzia uwezo wake wa kufanya kazi.
Mwalimu mstaafu wa shule ya msingi, Rehema Mathayo alisema kutokana na baadhi ya viongozi ndani ya CCM kukumbwa na kashfa za ufisadi, anayetaka kugombea urais lazima awe ‘msafi’ ndani na nje ya chama.
“Mshindi ndani ya chama ni mtu atakayekuwa amewashinda wenzake kwa kuwa na maadili mazuri na asiwe na doa lolote la kujishughulisha na ‘dili’ za ajabu,” alisema Rehema.
Mwalimu huyo aliongeza kuwa mgombea huyo lazima awe na uzoefu mkubwa wa masuala la kimataifa kwa kuwa hata kama atakuwa na maadili, kama hafahamu namna ya kuwaunganisha wananchi na jumuiya za kimataifa, hatakuwa na manufaa.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Ernest Mwasalwiba alisema kutokana na kuporomoka kwa maadili hususan kwa viongozi wa umma, vitendo vya rushwa na kadhia mbalimbali, rais ajaye anatakiwa kuhakikisha yale anayoyasema ndiyo anayatenda na Watanzania hawahitaji Rais dikteta.
“Masuala ya maadili, rushwa, yote haya yanazuiwa mpaka sasa lakini suala ni usimamizi tu... ni wakati sasa wa rais ajaye kuonyesha ajenda yake itakuwa ipi, anapokuwa amesema kitu kila mtu lazima afuate mfano akisema anachukia rushwa na maadili kwa yaheshimiwe isiwe ni mjadala kila mtu anafuata kuanzia chini hadi juu.
“Dikteta siyo kiongozi tunayemtaka, bali tunataka kiongozi atakayesimamia sheria na mifumo iliyopo iweze kufanya kazi ipasavyo... mfano Rais Jakaya Kikwete kipindi anaingia aliingia na kaulimbiu ya ‘Ari Mpya, Kasi Mpya na Nguvu Mpya’ ambayo ilifuatwa hadi na viongozi wa halmashauri.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe, Dk Romanus Dimoso alisema: “Sifa za rais huwa zinajulikana. Tunahitaji rais ajaye anayejua hali ya kisiasa ilivyo kwa sasa, hatutaki rais ambaye hatambui mchango unaotolewa na vyama vingi vya siasa na jinsi atakavyoweza kufanya navyo kazi hususan kwa kuhakikisha demokrasia inazingatiwa.”
Aliongeza: “Je, malengo ya anayetaka urais yale ya kuhakikisha ifikapo mwaka 2025 nchi hii inafikia uchumi wa kati. Amejipanga vipi kama mtumishi wa kwanza wa Taifa hili kutufikisha huko?... Hatutaki mtu awe rais tu kwa jina.”
Rais mstaafu wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dk Primus Saidia alisema: “Tunahitaji rais anayeweza kufanya uamuzi mgumu kwa mustakabali wa Taifa, asiwe rais wa maneno maneno, bali wa vitendo. Anasema dawa hospitalini hakuna na kesho zinakuwapo.
 “Tunataka mtu mwenye historia ya uongozi, ameshawahi kufanya nini katika kuboresha sekta ya afya, elimu, uchumi na kijamii? Alishafanya maamuzi magumu yapi ambayo kila mmoja aliyaona na aliyaheshimu?”
Asante kwa kutembelea blog hii ya Jambo Tz, ili kuboresha blog yetu tunatoa fulsa ya kutangaza matangazo mbalimbali na pia kutoa maoni yako kupitia namba ya simu (WhatsApp & SMS) 0715 221198, E-mail jambotz8@gmail.com. Merry Chistmass & Happy New Year.

Na Mwananchi 

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...