Friday, February 24, 2017

ZINGATIA: UKIPATA AJALI KWENYE CHOMBO CHA USAFIRI KAMA ABIRIA USIHANGAIKE KUPOTEZA MUDA KUTAFUTA MMILIKI, BALI FANYA HAYA.

 
MARA BAADA YA MATIBABU (Kupata nafuu au kupona)
 
1. NENDA  KATIKA KITUO CHA POLISI iliporipotiwa ajali ilikuweza kupata taarifa kuhusu ajali husika na jinsi ilivyoshughulikiwa. Taarifa hizo ni kama zifuatazo:

(a) Gari husika ilikatiwa bima kampuni gani?
(b) Je, ni hatua gani za kisheria zilizochukuliwa dhidi ya dereva wa gari husika. Kwa mfano alipelekwa mahakamani, kesi inaendelea au imeisha au bado anatafutwa au faili limefungwa. Kwa hatua yoyote kati ya hzo hapo juu kama imechukuliwa na polisi kutakuwa na nyaraka zinazoonesha jambo hilo.
(c) Kama kesi imekwisha, omba nyaraka za kesi hiyo kutoka polisi, zikiwemo nyaraka kuhusu ile gari na kampuni iliyoikatia bima. Baada ya hapo;

2. ANDIKA BARUA  kwenda kwa Meneja Mkuu/ Mkurugenzi au Meneja Madai(Claims Manager) wa kampuni husika ya bima. Ndani ya barua hiyo elezea kidogo ilivyokuwa, uliathirika nini kutokana na ajali au umeathirika nini na unadai nini au kiasi gani. KUMBUKA KWAMBA kiwango cha madhara uliyopata kwa mwili ndicho kitathmini au kutilia uzigo kiasi cha madai unachotaka kampuni ya bima ikulipe.

3. KATIKA BARUA hiyo utapaswa kuambatanisha:
(a)  cheti cha matibabu,
(b) tiketi ya safari (kama bado unayo, kama huna haina tatizo),
(c) Fomu ya polisi (PF 3, PF 115),
(d) Charge sheet na nakala ya hukumu (wengine huzitaka hizi)
(e) mchanganuo wa gharama ulizoingia kwa ajili ya matibabu na,
(f)  viambatanisho vyovyote,mfano picha za ulemavu wako, taarifa ya daktari zaidi ya PF3, kama ipo, ikiwamo gharama za usafiri wa kwenda na kurudi hospitali. Iwapo mhanga wa ajali hiyo amefariki basi itahitajika cheti cha kifo, na uthibitisho wa wewe kuwa msimamizi wa mirathi.
 
VINGINEVYO
Unaweza ukafuata utaratibu namba 1 tu hapo. Yaani ukaenda polisi ukakusanya nayaraka zako zote zinazohusina na hiyo ajali, kisha ukawasiliana na Mwanasheria wako kesi ikaelekea mahakamani. Lakini kesi hiyo haitakuwa dhidi ya KAMPUNI YA BIMA bali kesi itakuwa dhidi ya Mmiliki wa chombo cha usafiri kilichopata ajali au kama chombo kilikuwa kinamilikiwa na kampuni basi itashtakiwa kampuni inayomiliki chombo hicho ambayo jina lake lipo kwenye kadi ya gari.
 
MAKOSA YA WATU WENGI.
Watu wengi sana waliopata ajali hasa kwenye mabasi kama abiria, hukimbilia kwa mmiliki kudai fidia. Jambo ambalo wakifika huko hawapati msaada wowote Zaidi ya kuzungushwa zungushwa tu, kutukanwa, kejeli n ahata saa nyingine kuitiwa mbwa. Hili ni kosa. 

Kama ajali imetokea na iliripotiwa polisi, ina maana polisi wana nyaraka na vielelezo vyote kuhusu hiyo ajali. Kwa hiyo mahala sahihi pa kuanzia ni Polisi na sio kwa MMILIKI. Utarudi kw ammiliki tu ikiwa itakuja kuthibitika kuwa mmiliki hakukatia bima chombo chake au bima inayoonekana kwenye chombo chake ni feki. Hapa sasa kesi itakuwa ni kati yako na mmiliki. 

Na hata kwa utaratibu huu usiende kwa mmiliki. Unachopaswa kufanya ni kutafuta taarifa sahihi za mmiliki huyo, yaani wapi anakaa, kadi ya gari, anwani yake, namba ya gari kisha wewe mwenyewe au kupitia kwa mwanasheria wako peleka kesi ya madai ya fidia mahakamani ukiwa na vielelezo vyote vinavyothibitisha kutokea kwa ajali na madhara uliyoyapata. Ni Imani yangu umeelewa.

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...