Friday, March 22, 2013

JK aziponda Simba, Yanga


RAIS Jakaya Kikwete amezipiga ‘kijembe’ klabu kongwe hapa nchini, Simba na Yanga, kutokuwa na maendeleo kisoka na kuiacha Azam FC, ikiwapiga kumbo kila idara huku wao wakiendekeza ushirikina mbele na migogoro.
Kikwete aliyasema hayo jana, wakati akiweka jiwe la msingi la klabu ya Azam iliyoko Chamazi nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.

Rais aliipongeza Azam kwa hatua ambayo imefikia, licha ya kuwa na uchanga katika soka na kuzipita klabu za Simba na Yanga.

Alisema endapo Azam inataka kupiga hatua na kuifikisha nchi mbali kwa kulitangaza jina la Tanzania, ifanye mambo yake bila kuzifuata timu kongwe na kudai kuwa itafika mbali kitaifa na kimataifa pia.
“Naamini mna uwezo wa kufika mbali katika ulimwengu wa soka, ila msiwe karibu na hizi timu, mtajikuta mnaishia hapahapa; wao mechi mechi moja wanatolewa,” alisema Kikwete na kuwafanya watu walioshuhudia hafla hiyo kuvunjika mbavu.
Aidha Kikwete alisema kutokana na mafanikio ambayo Azam wameyapata hadi sasa, ikiwemo uwanja na mambo mengine, imeonekana kama wao ndio vigogo na kusababisha kuogopwa na jamaa ambao wanajifanya wakubwa.
 “Mpaka sasa haionekani nani mkubwa, maana kuwa na wanachama wengi sio ishu na nyie nina imani mnaweza kulileta hili Kombe la Shirikisho nyumbani, najua timu kubwa zikiwa na mechi na nyie zinakuwa na wasiwasi, hivyo basi mpaka sasa nyie ndio mtasaidia soka la Tanzania kukua,” alisema Kikwete.

Alikwenda mbali zaidi na kuwataka Azam, kuacha kufuata vivuli vya hizo timu na kujisimamia wenyewe, kwa kuwa timu mbili kongwe zina wanachama wanaopiga kura kwa kuhongwa, sambamba na kutumia muda mwingi kulumbana, wakati hawana kitu wanachoingiza katika timu.

Alisema timu kubwa zikiambiwa kutumia Uwanja wa Chamazi, zinaanza kuleta maneno ya ajabu na kuongeza kuwa ushirikina haufai katika soka, cha muhimu ni kucheza mpira na sio kazi ya kuandaa kamati za ufundi na kushindwa kutazama benchi la ufundi ili kujenga timu.
“Ingekuwa mpira ni ushirikina, basi Afrika tungekuwa mabingwa kila mwaka, kama timu inaona uchawi dili, basi ikusanye wachawi wote dunia nzima ikae nao klabuni kwao tuone!” aliongeza Kikwete.

Aliwataka Azam endapo watakuwa na shida yoyote, wasisite kumjulisha na kudai kuwa ombi lao la kupunguziwa VAT katika bidhaa zao za kisoka, atawasiliana na wahusika ili aweze kulipatia ufumbuzi.
Naye Mkurugenzi wa Azam, Yusuph Bakhressa, alishukuru sana kupata nafasi ya Rais kuzindua mradi wao maalumu, ambao lengo lake ni kukuza na kuendeleza mpira wa miguu nchini.
Alisema hadi sasa wametumia sh bilioni 3 katika mradi huo.
Katika hafla hiyo, Rais aliambatana na mkewe Mama Salma Kikwete, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam, Mecky Saidi Sadick, na viongozi mbalimbali.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...