Thursday, November 14, 2013

CCM YATOA POLE MSIBA WA DR.SENGONDO MVUNGI


 KINANA_MKUTANO_WA_SHIRIKISHO_LA_CCM_VYUO_VIKUU_MORO_PIX_NO_2_529d1.jpg
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Ndugu Abdulrahaman Kinana amesikitishwa na taarifa ya kifo Cha Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Dr Sengondo Mvungi kilichotokea Jana katika Hospitali ya Millpark nchini Afrika ya Kusini.

Kwa niaba ya Chama Cha Mapinduzi, Katibu Mkuu anawapa pole wanafamilia, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Warioba na Uongozi wa Chama Cha NCCR-Mageuzi. Hakika Taifa limepoteza Mtaalamu wa Sheria, Kiongozi Mzalendo na hodari katika kipindi ambacho mawazo yake yanahitajika kwa kiasi kikubwa kuliendeleza Taifa hili.
Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema peponi.

Imetolewa na:
KATIBU WA HALMASHAURI KUU YA TAIFA
ITIKADI NA UENEZI
13/11/2013
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha mjumbe wa tume ya mabadiliko ya katiba Dr Sedondo Mvungi ambacho kimetokea katika hospitali ya Millpark nchini Afrika kusini.

Uongozi wa UVCCM Taifa unatoa pole kwa familia na ndugu wa marehemu, pia UVCCM inatoa pole kwa uongozi wa NCCR- Mageuzi na kwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Warioba pamoja na Vijana nchini kote ambao wamenufaika na Utaalamu na mafunzo. 
Kama vijana tulihitaji sana mchango wa mawazo, hekima na utaalamu kutoka kwake, hakika tumepoteza kiongozi shupavu, muadilifu na mzalendo ambae ni mfano wa kuigwa kwa Vijana wa Taifa hili.

Kadhalika, UVCCM inatoa pongezi za dhati kwa hotuba makini iliyojaa hekima, busara na ushupavu wa Uongozi iliyotolewa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete.

Hakika vijana tumeridhishwa na maamuzi ya Mheshimiwa Rais ya Kuendelea kuwa Mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na tunapongeza maamuzi hayo yanayolenga kudumisha Umoja na Ushirikiano wa Nchi za kiafrika katika kujiletea maendeleo. Kwa kutambua nafasi na manufaa yanayopatikana kwa vijana kutokana na fursa za kiuchumi, kisiasa, kijamii, ajira nk UVCCM Inamuunga mkono Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake huo.

Pamoja na kuunga mkono uamuzi huo, UVCCM inatoa angalizo kuwa ni vyema kwa nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kuendelea kuheshimu taratibu na kanuni za jumuiya hiyo ili kuifanya endelevu, imara na mfano kwa nchi nyingine za Afrika na Duniani kwa ujumla. Ni lazima wazingatie kuwa Umoja na Mshikamano ndio nguzo ya maendeleo ya kweli ya Afrika.

Pia, Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) umesikitishwa na tuhuma ambazo zimeripotiwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari kutoka kwa Mbunge wa Arusha Mjini (CHADEMA) Mheshimiwa Godbless Lema ambazo amezielekeza kwa baadhi ya Viongozi wa Jumuiya akiwemo Mwenyekiti wa Taifa wa UVCCM Ndugu Sadifah Juma kuwa amehusika na usambazaji wa Picha chafu mitandaoni.

Pamoja na kusikitishwa, UVCCM inazo taarifa juu ya mgogoro unaoendelea katika Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na kwamba inamtaka Lema kutoelekeza tuhuma kwa UVCCM na viongozi wake bali waangalie namna bora ya kushughulikia na kutatua migogoro yao ya ndani ambayo imesababisha kuzushiana, kuchafuana na kuvujishiana siri katika mitandao hasa ya kijamii.

UVCCM na Viongozi wake inakana kwa namna yeyote ile kuhusika na usambazaji huo na kwamba Jumuiya hii ni ya Vijana makini na wanaojitambua na inajielekeza katika kufanikisha malengo ya kuundwa kwake ya kukisaidia Chama kushika dola mwaka 2015.
Na kwamba UVCCM inalaani tabia ambayo imeasisiwa na Vijana wa CHADEMA ya kukashifu, kuzomea na hata kutukana Viongozi wa CCM na Serikali yake na kwamba yaliyomkuta Mhe Lema ni matunda ya kazi waliyoiasisi wenyewe.
Imetolewa na:
PAUL MAKONDA
KATIBU WA IDARA YA HAMASA NA CHIPUKIZI
UVCCM
13/11/2013

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...