Tuesday, November 11, 2014

POLISI YAWATAWANYA WAFUASI WA MBOWE KWA MABOMU


Mwenyekiti wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (chadema), Freeman Mbowe 

Wafuasi wa (Chadema) wilayani Mpanda jana jioni walilazimika kutafuta vichochoro vya kukimbilia baada ya polisi kusambaratisha kwa mabomu ya machozi, maandamano ya kumsindikiza Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe baada ya mkutano.

Patashika hiyo ilitokea baada ya mkutano wa Mbowe kumalizika na wafuasi wake kutaka kumsindikiza hotelini, jambo ambalo polisi hawakulikubali.

Baada ya wananchi hao kuanza maandamano hayo, polisi walifyatua mabomu takriban 15 yaliyowafanya wafuasi wote kutawanyika na kusababisha taharuki miongoni mwa wakazi wa mji huo. Dakika chache baada ya tukio hilo, umeme ulikatika mji mzima.

Tofauti na maeneo mengine aliyofanya ziara zake kama Tabora, Sikonge na Igunga ambayo wafuasi walikuwa wakimsindikiza, polisi wa Mpanda walijipanga ipasavyo tangu mapema kuhakikisha hali hiyo haitokei. Asante kwa kutembelea blog hii na endelea kuwa nasi siku zote, kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Kabla ya rabsha hizo, Mbowe alikuwa katika Jimbo la Mpanda Mjini, linaloongozwa na Said Arfi (Chadema) ambaye alimwelezea kama mwanamapinduzi aliyekisaliti chama.

Mbowe aliyezungumzia usaliti huo kwa mifano, alisema safari ya mapinduzi ya Arfi ilikuwa kama ya treni kutoka Dar es Salaam hadi Mpanda lakini mbunge huyo aliteremkia njiani. “Arfi ni mtu wa kujipendekeza anayependa kunywa chai na vigogo wa CCM. Hivi mnachukuliaje kushushwa njiani kwa Arfi katika safari ya mapinduzi?” aliwahoji wafuasi waliohudhuria mkutano huo.

Wafuasi hao walijibu kuwa hawajali usaliti huo na kwamba safari ya mapinduzi inaendelea na wanataka mbunge imara asiye mwoga.

Alipoulizwa kuhusu madai dhidi yake, Arfi alisema yeye ni mtu mzima, nafsi yake inamwelekeza anyamaze kimya.

Baada ya kufika katika mkutano huo, Mbowe alisema alichelewa kidogo kwa sababu alikuwa analipitia jimbo la Waziri Mkuu Mizengo Pinda alilodai: “Limekithiri kwa uvunjaji mkubwa wa haki za binadamu.”

Alikuwa anazunguka kwa helikopta katika jimbo hilo na alizungumza na wananchi walioathirika na Operesheni Tokomeza ambao walimfahamisha kuwa bado wanaendelea kudhulumiwa mifugo yao.

“Baadhi ya watu walichomewa mifugo yao na hadi sasa hawajalipwa na bado wanaendelea kufanyiwa vurugu lukuki na ya mifugo yao. Kama hayo yanaendelea katika jimbo la Waziri Mkuu je, katika maeneo mengine yatakuwaje?” alihoji Mbowe.

Kutokana na hali hiyo, mwenyekiti huyo aliwataka wananchi hao kuchukua hatua dhidi ya viongozi wanaoshindwa kuzuia maovu ili yasitokee tena.
 Wafuasi wa chama hicho walilalamika kuwa hawakutendewa haki kwani viongozi wa CCM walikuwa wakisindikizwa bila polisi kuwatawanya na walitolea mfano wa ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana aliyoifanya mkoani hapo na kusindikizwa na wafuasi wake bila polisi kuingilia. Asante kwa kutembelea blog hii na endelea kuwa nasi siku zote, kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Na Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...