Wednesday, September 24, 2014

ESTER BULAYA ATANGAZA VITA NA WASIRA...!!!




Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Mkoa  wa Mara, Ester Bulaya akizungumza  katika mahojiano maalumu na waandishi wa gazeti hili, Dar es Salaam jana.

Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Ester Bulaya ametangaza rasmi nia ya kugombea ubunge katika Jimbo la Bunda ambalo linashikiliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira.

Kwa nia hiyo, Bulaya anaweza kuwa ametangaza vita dhidi ya Wasira ambaye hivi karibuni akiwa Bunda, alitangaza kukitetea kiti chake hicho katika Uchaguzi Mkuu 2015.

Julai 8, mwaka huu Wasira akiwa kwenye kikao cha kawaida cha Halmashauri Kuu ya CCM wilayani Bunda, alitangaza kuwa atatetea nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu ujao, huku akijigamba kuwa yeye ni “mwarobaini wa matatizo” yanayowakabili wakazi wa jimbo hilo.

Kabla ya kutangaza nia hiyo, mara kadhaa Wasira amekuwa akihusishwa na suala la urais na ni mmoja wa makada sita wa CCM ambao walipewa adhabu na chama hicho Februari 18 mwaka huu, baada ya kukutwa na makosa ya kuanza mapema kampeni za urais mwaka 2015.

Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili jana, Bulaya alisema atagombea ubunge katika Jimbo la Bunda na anamtakia kila heri mpinzani wake huyo (Wasira) katika nafasi ya juu ya urais anayotaka kuwania. Alisema ameamua kufanya hivyo baada ya kuombwa na watu kadhaa kutoka jimboni humo wakiwamo vijana, wazee na kinamama. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

“Ninaamini nimepata uzoefu mkubwa katika kipindi hiki cha ubunge wa viti maalumu na ninawataka wabunge wenzangu wa viti maalumu waone kuwa nafasi hiyo ni fursa ya kujifunza, lakini mwisho wa yote lazima urudi jimboni,” alisema.

“Hii ni mara ya kwanza nasema hapa. Nitagombea ubunge Jimbo la Bunda kwa kuwa nimeombwa sana na vijana, wazee na ni mara nyingi nimekuwa nikisema bado muda, lakini sasa umebaki muda mfupi hivyo niseme tu kwamba nitagombea. Uongozi ni mbio za kupokezana vijiti. Wasira ni kama baba yangu na sina ugomvi naye na namtakia kila la heri katika position (nafasi) yake nyingine anayoitaka,” alisema.

Kuhusu madai kwamba Wasira anafikiria kuwania urais, alisema, “Naona ni uamuzi sahihi amefanya, kwani amekuwa mbunge tangu mimi nazaliwa mwaka 1980 ameona kwamba ni kweli hii position (nafasi) ya chini ameshaitumikia sana, hivyo ameona katika uzoefu alionao labda ajaribu katika nafasi ya urais.”

Bulaya alisema si kwamba ameamua kugombea ubunge wa Bunda kwa kuwa Wasira anataka urais, bali viti maalumu alipo hivi sasa ni njia ya kupata uzoefu na kujifunza katika kuelekea kugombea ubunge wa jimbo.

“Ili kuondoa suala la kwamba viti maalumu ni vya kupewa siyo kwamba nasema vifutwe, lakini unaweza ukawekwa utaratibu mwingine wa kumpa mwanamke uzoefu katika ngazi ya kibunge,” alisema na kuongeza;

“Lakini unapopewa hebu itendee haki hiyo fursa, kama mtu umeingia viti maalumu unajifunza na unakwenda kugombea na huko kuna kushinda na kushindwa lakini ni lazima nionyeshe hii fursa nimepewa naweza kwenda kushindana na wanaume.”

Alisema hilo ni jambo la msingi kwa kuwa huwezi kulemaa kwa kuwa mbunge wa viti maalumu bila kujifunza na kukaa miaka hadi 15 kwenye ubunge wa aina hiyohiyo kwani wako wengine wanaotakiwa kupata nafasi hiyo ili wajifunze na kwenda majimboni.
“Katika kushindana kuna mawili na lazima ujiandae kwa yote ingawa mwisho wa siku wananchi ndiyo wanaona huyu ana uwezo, tumempa dhamana ya viti maalumu ameitendea haki nafasi hiyo,” alisema.
Uamuzi mbovu
Alipoulizwa ni jambo gani lililowahi kumkera alilofanya yeye au chama chake katika kipindi cha ubunge wake, Bulaya alitaja mabadiliko ya Baraza la Mawaziri yaliyowaondoa waliokuwa mawaziri; Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii), Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa), Dk Emmanuel Nchimbi (Mambo ya Ndani) na Dk Mathayo David Mathayo (Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi) akisema huo ni uamuzi wa kujutia. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz
“Ninajutia ‘party caucus’ iliyowaondoa mawaziri kutokana na Operesheni Tokomeza Ujangili, kwani waliotakiwa kuwajibika ni watendaji na si mawaziri wale. Naamini hao walitolewa kafara kwa sababu.
Naamini waliopaswa kushughulikiwa walikuwa watendaji na siyo mawaziri,” alisema.
Alisema aliumia kwa kuwa haiwezekani watendaji wafanye makosa halafu wanaendelea kubaki lakini mawaziri wachapakazi wakaondolewa na kwamba hilo lisiporekebishwa, wataendelea kutolewa kafara na mawaziri ambao ni wachapakazi... “Haya mabadiliko hayakunifurahisha kwa kweli.”
Mbio za urais
Alipotakiwa kutoa maoni yake juu ya wanaojitokeza kuwania urais, Bulaya haoni kati yao mwenye sifa ya kuwania nafasi hiyo ya juu ya uongozi.
Ingawa hakutaja jina la mtu, Februari 18 mwaka jana 2013, Kamati Kuu ya CCM iliwafungia makada sita wa CCM, ambao ni Bernard Membe, Frederick Sumaye, Edward Lowassa, Stephen Wasira, January Makamba na William Ngeleja baada ya kuwabaini kuwa walikuwa wameanza kampeni za urais kabla ya wakati.
Tamko la Kamati Kuu ya CCM lilisema: “Waliohojiwa wamethibitika kuwa na makosa yafuatayo: Kuanza kampeni za kutafuta kuteuliwa kugombea urais kabla ya wakati kinyume na kanuni za uongozi na maadili za CCM Toleo la Februari 2010 Ibara 6 (7), kufanya vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya chama na baadhi yao kufanya vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya jamii. Kosa hilo nalo ni kwa mujibu wa Kanuni za Uongozi na Maadili za CCM Toleo la Februari 2010 Ibara kadhaa za kanuni hizo.”
Bulaya alisema, “Kutaka urais ni jambo moja na kuchaguliwa na ni jambo jingine. Itafika muda Watanzania watasema nani anafaa, lakini mimi naamini kuna makada wengi wenye sifa kuliko hao, ambao hawajajitokeza na pengine hawatajitokeza kabisa. Katika nafasi ya urais hatuhitaji watu ambao Mwalimu Nyerere aliwakataa kwa kuwa ni wala rushwa na wanaotumia madaraka vibaya. Katika mchakato huo wa Katiba kumejitokeza maoni ya watu kwamba huyo anafaa na yule hafai. Lakini kikubwa ni kuangalia watu wenye hulka ya Mwalimu Nyerere.”
“Kimsingi mimi nakereka sana ninaposikia watu wakihusisha urais na umri. Umri hauwezi kuwa sifa ya urais. Rais anapaswa kuwa mtu anayejua changamoto na udhaifu wa uongozi uliopita, ajue tatizo la Taifa, achukie matumizi mabaya ya madaraka na aguswe na umaskini wa Watanzania.
“Sifa nyingine ni mtu kuwa na uwezo wa kuondoa tabaka la matajiri na maskini, kuheshimu misingi ya utawala bora na akatae rushwa kwa vitendo.”
Alipoulizwa kama anaona upinzani una fursa katika nafasi hiyo ya juu serikalini, Bulaya alisema, “Naamini CCM bado ina fursa nzuri, ila isibweteke kwa kuwa Watanzania wa leo siyo wajinga.”
Alisema CCM haipaswi kuudharau upinzani, badala yake ishughulikie changamoto zinazotolewa na upande huo wa pili kwa ajili ya kuboresha maisha ya Watanzania ili iendelee kuaminika. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Na Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...