Wednesday, September 24, 2014

KINANA, NAPE WAKERWA NA MASHINE ZA EFD NA BVR




Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akisalimiana na wazee wa Kijiji cha Kwenjugo, Handeni jana, akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake mkoani Tanga.

Chama Cha Mapinduzi kimeonyesha wasiwasi kuhusu matumizi ya teknolojia ya kielektroniki katika uandikishaji wa wapigakura na mashine za ukusanyaji wa kodi (EFD).

Wasiwasi huo umeelezewa kwa nyakati tofauti na Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye wakati wakihutubia mkutano wa hadhara katika Mji Mdogo wa Chalinze, wilayani Bagamoyo juzi.

Kinana alihoji utaratibu aliouita mbovu katika matumizi ya mashine za kielektroniki za kutunza hesabu za wafanyabiashara (EFD) na Nnauye alieleza wasiwasi wake kuhusu uamuzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kutumia teknolojia ya Biometric Voter Registration (BVR) katika kuandikisha upya wapigakura.

Nnauye aliishauri Nec kuangalia upya uamuzi wake huo akisema hauna mantiki kwa kuwa utaliingizia Taifa gharama ambazo zinaweza kuepukwa kwa urahisi.

Teknolojia hiyo iliwahi kulalamikiwa bungeni na Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe katika hotuba yake ya bajeti mwaka jana, akisema NEC imeanzisha utaratibu huo bila kuwashirikisha wadau.

Akitoa mifano, Nnauye alisema matumizi ya teknolojia hiyo yalizua mtafaruku katika chaguzi za nchi za Kenya, Malawi na Ghana na haitakuwa busara Tanzania nayo kujiingiza kwenye matatizo kama hayo wakati ina uwezo wa kuyaepuka. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

“Tatizo ni kuwa Tume (Nec) inataka kuandikisha wapigakura upya kwa kuchukua taarifa zao za kibaiolojia wakati taarifa kama hizo tayari zimeshachukuliwa na taasisi nyingine. Litakuwa jambo rahisi na lisilo na gharama kubwa kwa Tume kukaa na taasisi hizo na kuchukua taarifa hizo na kuziingiza katika majina ya wapigakura ambao tayari wameshaandikishwa. “Ikishafanya hivyo, Tume itabakiwa na kazi moja tu ya kuandikisha wapigakura wapya ambao bado hawajaandikishwa na idadi yao inakadiriwa kuwa kama milioni tatu hivi,” alisema Nnauye.

Alizitaja taasisi ambazo zinachukua alama za vidole wakati wa kutoa vitambulisho kuwa ni Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida), Mamlaka ya Usajili wa Vizazi na Vifo (Rita), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Idara ya Uhamiaji.

“Kama NEC wanataka kupata alama za vidole za wapigakura ni jambo rahisi la kukaa na mamlaka hizi na kupata taarifa hizo... tusipoangalia Tanzania inaweza kuweka rekodi ya kuwa nchi ya kwanza barani Afrika kuwa na taasisi nyingi zinazochukua wananchi wake alama za vidole,” alisema.

Alisema wakati Serikali ikitenga Sh7 bilioni tu katika bajeti yake ya mwaka huu kwa ajili ya uandikishaji wa wapigakura, Nec ilikuwa imeomba takriban Sh200 bilioni kwa ajili ya kazi hiyo.

Hata hivyo, juzi Mwenyekiti NEC, Jaji Damian Lubuva alisema tayari Tume hiyo imepokea Sh290 bilioni kutoka serikalini kwa ajili ya ununuzi wa vifaa hivyo na gharama nyingine za mchakato wa uboreshaji daftari la wapigakura.

Nape alisema CCM imeamua kutoa hadhari na ushauri huo kwa sababu ipo hatari iwapo uchaguzi utavurugika kutokana na Tume kung’ang’ania matumizi ya teknolojia hiyo, wapinzani wanaweza kukinyooshea kidole chama hicho na kukituhumu kuwa kimehujumu.
Matumizi ya EFD
Kinana alihoji utekelezaji wa matumizi ya mashine za EFD na kubainisha kuwa una kasoro nyingi.
Alisema hana matatizo na uamuzi wa kutumia mashine hizo, bali utaratibu uliotumika katika kuanzisha matumizi yake.
“Naomba waandishi wa habari mnielewe vizuri katika hili. Sina matatizo na uamuzi wa kutumia hizi mashine, lakini utaratibu unaotumika kuzitumia ndiyo una matatizo na hilo si sawa,” alisema.
Alisema baadhi ya malalamiko ya wafanyabiashara ni ya msingi na yanapaswa kutafutiwa ufumbuzi.
Aligusia suala la bei za mashine hizo kama moja ya matatizo yaliyojitokeza... “Zilipoingizwa kwa mara ya kwanza wafanyabiashara wakauziwa kwa Sh4 milioni. Wakalalamika bei ikapungua hadi Sh2 milioni, walipolalamika tena ikashuka zaidi hadi Sh800,000 wakazidi kulalamika bei ikashuka hadi Sh600,000. Sasa mtu unajiuliza hivi bei halisi ya mashine hizi ni ipi?”
Kinana alihoji, wakati TRA inawataka wafanyabiashara kuzinunua mashine hizo kwa fedha zao kurudishwa kidogo kidogo kama makato pungufu katika kodi wanazolipa, mfanyabiashara akifilisika kabla fedha alizotumia kununulia hazijarejeshwa zote ni nani atamfidia?
Alisisitiza kuwa kuna upungufu katika sheria inayohusu matumizi ya mashine hizo na wafanyabiashara wanaopinga wasionekane ni wakorofi... “Watu wakibisha wanaambiwa wanavunja sheria wakati sheria yenyewe imepinda.”
Serikali ilianzisha matumizi ya EFD kama moja ya mikakati ya kupanua wigo wa walipakodi ili kuongeza mapato yake na kuongeza uwezo wa kugharimia matumizi yake kwa fedha za ndani. Inakadiriwa kuwa watu wanaolipa kodi nchini milioni mbili kati ya milioni 15 wanaostahili. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Na Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...