Thursday, March 12, 2015

KONTENA LALALIA BASI, LAUA WATU 42, LAJERUHI 23

Basi la Majinja likiwa limeangukiwa na kontena na kusababisha vifo katika eneo la Changalawe mafinga.

Watu 42 wamepoteza maisha na wengine 23 kujeruhiwa baada ya lori la mizigo kugongana na basi na kontena lililokuwa limebebwa kuangukia gari hilo la abiria, katika ajali ya aina yake iliyotokea eneo la Mafinga Changalawe mkoani Iringa.
Watu 37 waliokuwa kwenye basi hilo la kampuni ya Majinjah Express lililokuwa likitokea Mbeya kwenda Dar es Salaam, walifariki papo hapo na wengine watano kufariki wakiwa Hospitali ya Mafinga. Dereva wa basi na wa lori hilo la kampuni ya Cipex, pia wamefariki.
Shuhuda mmoja wa ajali hiyo, Nyasio Pascal, aliyekuwa akiendesha basi la Saibaba, alisema aliliona lori hilo likijaribu kukwepa mashimo kwenye barabara hiyo ambayo ni nyembamba, na mara likaanza kuyumba kulia na kushoto baada ya kukanyaga shimo na ndipo lilipolifuata basi na kugongana nalo.
Alisema kontena lililokuwa limebebwa na lori hilo, liliangukia juu ya basi na kulikandamiza, jambo ambalo lilisababisha vifo vya watu wengi na pia kuzuia watu waliokuwa karibu na ajali kuokoa watu waliojeruhiwa hadi tingatinga lilipowasili. Hata hivyo, alisema mtoto mmoja mwenye umri wa mwaka mmoja, alinusurika kwenye ajali hiyo bila ya kudhurika. Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.
Miili ya waliokufa imehifadhiwa kwenye Hospitali ya Mafinga, ambayo ina chumba cha kuhifadhia miili ya watu saba tu, na mingine imepelekwa Hospitali ya Rufaa ya Iringa.
“Hii ni ajali mbaya ambayo haijawahi kutokea mkoani hapa,” alisema mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza aliyefika eneo hilo la ajali.
Wanaume saba na wanawake 35 wamepoteza maisha kwenye ajali hiyo, iliyochukua maisha ya watoto watatu.
Katika eneo hilo ambako ajali hiyo imetokea hali ilikuwa mbaya kutokana na kontena la lori hilo kulalia basi na kukandamiza miili ya abiria, jambo ambalo lilisababisha ugumu katika kuokoa abiria waliokuwemo ndani ya basi.
Polisi wakishirikiana na watoa huduma ya afya kutoka Mufindi walifika kusaidia katika kutoa huduma ili kuokoa wale ambao walikuwa wamejeruhiwa na kuhitaji matibabu ya haraka.
Tingatinga lilifika na kusaidia kulinyanyua kontena na hivyo kurahisisha kazi ya kutoa miili ya wale waliokuwa wamebanwa na miili ya waliokufa pia.
Majeruhi wazungumza
Kevin Humprey, aliyekuwa amekaa viti vya nyuma kwenye basi hilo, alisema alisikia kishindo kimetokea na kuona kontena limelalia sehemu kubwa ya basi.
“Baada ya kuona hivyo, nilianza kupiga kelele za kuomba msaada kwa kuwa tulikuwa porini,”alisema Humprey.
Abiria mwingine aliyekuwa amekaa viti vya nyuma, Josam Obel, alisema alishtukia tu kontena likiwa limelalia gari lao.
Alisema lori lililokuwa linakwenda Mbeya liliacha njia kutokana na mashimo yaliyokuwepo barabarani na kugongana uso kwa uso na kusababisha kontena lililokuwa limebebwa na lori kuangukia kwenye basin a kulikandamiza.
Alisema basi hilo lilikuwa na abiria wengi kuliko uwezo wake kwa kuwa lina uwezo wa kubeba abiria kati ya 50 na 54, lakini lilibeba zaidi ya abiria 60.
Hali mbaya katika Hospitali ya Mufindi
Hali katika Hospitali ya Wilaya ya Mufindi ilikuwa mbaya kutokana na watu wengi kufurika kutaka kujua kama ndugu zao ni kati ya hao walikufa au kujeruhiwa kwenye ajali hiyo.
Vilio vilitanda kila kona ya hospitali hiyo hasa wakati miili ya waliokufa ilipokuwa ikishushwa na kuwekwa eneo maalumu kwa ajili ya utambuzi, jambo lililofanya kazi hiyo kuwa ngumu kutokana na kila mtu kutaka kuona maiti hizo. Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.
Mganga mfawidhi wa hospitali hiyo, Boaz Mnenegwa alisema walipokea miili ya watu 37 ambao walikufa kwenye ajali na kwamba wengine watano walifia hospitalini.
Alisema majeruhi 23 walifikishwa hospitalini hapo na kati yao watano walifariki na wengine zaidi ya 10 wamepelekwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa.
“Majeruhi hao wameumia maeneo mbalimbali ya mwili ikiwemo kichwani, miguuni na mikononi,” alisema.
Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Iringa, Ramadhani Mungi alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa magari hayo mawili.
Alisema madereva wa magari yote waliofahamika kwa majina ya Baraka Gabriel wa basi na Makka Sebasian wa lori walikufa papo hapo na haikuweza kujulikana idadi ya watu waliokuwamo kwenye lori hilo.
Hata hivyo, Kamanda Mungi alisema ni vigumu kupata majina ya waliokufa na majeruhi kutokana na shughuli za kutafuta kuendelea ili kuweza kuwatambua.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alisema kuwa ajali hiyo ni mbaya ambayo haijawahi kutokea katika mkoa huo
“Tuko hapa kwa ajili ya kuhifadhi maiti na kutambua ndugu wa marehemu,” alisema.
Masenza aliongeza kuwa barabara hiyo imekuwa na ubovu kila mara, hasa wakati wa mvua inapochimbika na kuweka mashimo ambayo yalichangia ajali ya jana kwa sababu gari zote zilikuwa zikipishana na kukwepa mashimo hayo.
Dereva wa basi la Saibaba, Nyasio Pascal aliungana na mkuu huyo wa mkoa akisema: “Sisi kama madereva ambao tunatumia barabara hii, kiukweli tunakerwa na kipande hiki cha barabara kwa sababu ya mashimo na ni finyu hamuwezi kupishana kwa hiyo ajali hii imetokea kwa sababu ya ubovu wa barabara,” alisema. Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...