Wednesday, September 10, 2014

YANGA HIYOOOO MPAKA FIFA

Kwa maana hiyo Okwi ni mchezaji huru, hivyo yuko huru kujiunga na timu yoyote.

Uongozi wa Yanga umepanga kuliandikia Shirikisho la Kimataifa la Soka (Fifa) kuishtaki TFF kwa kukiuka Kanuni ya 19 ya usajili katika kufanya uamuzi wa utata wa usajili wa mshambuliaji wa Uganda, Emmanuel Okwi.
Kikao cha Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF kilichofanyika jijini Dar es salaam juzi, kiliamua kumtangaza Okwi kuwa mchezaji huru baada ya kubaini kuwa Yanga ilivunja mkataba kwa kutomlipa stahiki zake za usajili na pia kuandika barua TFF kutaka mkataba wake na Mganda huyo uvunjwe, uamuzi ambao umeinufaisha Simba ambayo imemsajili.
Mkataba wa mchezaji huyo ulipitiwa na kamati hiyo ikiwamo kumsikiliza mchezaji mwenyewe pamoja na Yanga na kuridhika kuwa mkataba kati ya pande hizo umevunjika.
Kamati hiyo ilisema ukiwa ni mkataba wa pande mbili, Yanga ilikiuka kipengele namba nane kuhusu malipo ya ada ya usajili. Yanga ikiwa mwajiri, haikutekeleza kipengele hicho hadi kufikia Juni 27 mwaka huu, ilipoandika barua TFF kuomba mkataba huo uvunjwe. Kwa maana hiyo Okwi ni mchezaji huru, hivyo yuko huru kujiunga na timu yoyote.
Hata hivyo, uongozi wa Yanga jana ulisema haukubaliani na uamuzi huo na kwamba walikuwa wameshaandika barua kupinga baadhi ya wajumbe katika kamati ya sheria ya TFF wasisikilize kesi yao, akiwamo mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Pope ambaye pia ni mjumbe wa kamati hiyo ya sheria.
Akizungumza jijini jana, mwenyekiti wa Kamati ya Sheria na Katiba wa Yanga ambaye pia aliiwakilisha Yanga juzi, Sam Mapande alisema hawana imani na kamati iliyotoa uamuzi kwa kuwa kuna mgongano wa kimasilahi na TFF wanajua hilo.
“Msimamo wetu ni kwamba tunatambua Okwi bado ni mchezaji wetu kwa kuwa tuliwaandikia barua TFF ya kuvunja mkataba na Okwi hawajafanya hivyo, kuna wajumbe tuliomba watoke, lakini hawakutoka hivyo hatuna imani na kamati. Pia TFF ilipaswa kusaka wasuluhishi wengine ambao si wa kamati ile kwa sababu tayari tulishaonyesha wasiwasi, lakini TFF haikufanya hivyo,” alisema Mapande.
“Jana (juzi) tumetoka pale tukikubaliana na kamati leo (jana) tupeleke maelezo mengine ya ziada kama tunayo, lakini tunasikitika wametoa uamuzi wakati hatujawasilisha maelezo yetu.
“TFF walikuwa na ajenda zao binafsi kwani licha ya kuwapelekea barua lukuki hakuna hata moja iliyofanyiwa kazi zaidi kuandikiwa barua ya kuitwa kwenye kikao cha jana (juzi).
“Barua ya TFF ilituambia itajadili malalamiko yetu yote ikiwamo ya Okwi kufanya mazungumzo na timu ya Misri kinyume cha taratibu, itajadili barua ya Yanga kuomba kuvunja mkataba na Okwi na barua ya kumlazimisha arudishe fedha zote za usajili na mishahara aliyochukua, pia alipe Dola 200,000 kwa kuikosesha Yanga ubingwa.
“Tuliishtaki pia Simba na timu ya Misri kufanya mazungumzo na Okwi kinyume cha taratibu. Lakini cha kushangaza tulipoingia kwenye kikao, yule mwenyekiti (Richard Sinamtwa) alisema wanashughulika na usajili tu na si malalamiko mengine. Hiyo ni ajabu sana,” alisema Mapande.
Alisema: “Kamati ya Sheria ya TFF imejivika malalamiko kwa kutolea uamuzi jambo ambalo halikuwapo mezani mwake. Kwenye mkataba kuna kipengele kinasema mkataba unavunjwa kwa pande mbili kuelewana kama wameshindwana kimkataba, lakini Okwi hakuwahi kupeleka malalamiko yoyote TFF.”
Hata hivyo, Kaimu katibu mkuu wa TFF, Boniface Wambura alisema kuwa masuala ya uhalali wa Okwi kusajiliwa Yanga au Simba yataamuliwa Jumamosi wakati kamati ya sheria na hadhi ya wachezaji itakapokutana kwa mara nyingine kupitia masuala ya usajili.
Wakati huohuo, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Pope amesema Yanga waende wanapoenda ila wataishia kuhangaika kwani Kamati ya Sheria TFF imetoa uamuzi sahihi bila kupepesa macho kwamba Okwi ni mchezaji huru na hivi sasa ameamua kujiunga Simba ambayo aliwahi kuichezea kabla ya kwenda Tunisia kuitumikia klabu ya Etoile du Sahel.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...