Tuesday, June 17, 2014

CHENGE: "SERIKALI IMEKOSA UBUNIFU"


Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge. PICHA|MAKTABA 

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge amesema Serikali imekosa ubunifu na haitaki kupokea ushauri kuhusiana na vyanzo vipya vya mapato ya uchumi kwa mwaka 2013, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2014/15 pamoja na utekelezaji wa Bajeti kwa mwaka 2013/14, Chenge alisema kuongeza ushuru katika bia, soda, juisi na vinywaji vikali, kumepitwa na wakati.

Wakati Chenge akieleza hayo, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imetaja vyanzo mbadala vya mapato vinavyofikia Sh6 trilioni. Katika taarifa yake, Chenge alisema mpaka mwisho wa mwaka wa fedha 2013/14, Bajeti ilikuwa pungufu kwa Sh2 trilioni, huku Bajeti ya mwaka 2014/15 ikiongezeka kwa asilimia 8.8 (trilioni 1.6), huku ikiwa na deni la Sh1.3 trilioni ambalo halikuingizwa katika Bajeti ya mwaka 2014/15.
“Hali hii inaweza kutafsiriwa kuwa Bajeti ya mwaka 2014/15 tayari ina pengo la Sh4.9 trilioni. Yaani Sh2 trilioni ambazo hazikupatikana mwaka wa fedha 2013/14 na Sh1.6 trilioni ambayo imeongezeka ikilinganishwa na bajeti ya mwaka jana na deni la Sh1.3 trilioni.
“Kuna umuhimu wa kuharakishwa kuletwa bungeni sheria ya bajeti itakayofanya kazi sambamba na sheria mpya ya ununuzi ili kudhibiti matumizi mabaya kwa nia ya kuweka nidhamu katika utekelezaji wa bajeti ya Serikali,” alisema Chenge. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz
Alisema wakati Serikali ikiwa haina vyanzo vya uhakika vya mapato, Deni la Taifa lililofika Sh30 trilioni sawa na asilimia 57 ya pato la taifa ni mzigo wa taifa na tishio kwa utengamavu wa uchumi jumla.
“Uwiano uliopo wa Deni la Taifa na Pato la Taifa kiuchumi siyo wa kuridhisha. Ukubwa wa deni hili hauwiani na kiwango cha uzalishaji mali na ukuaji wa uchumi wa sasa wa asilimia 7.0,” alisema na kuongeza:
“Yalifanyika manunuzi ya Dola za Marekani 810,000 katika Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ambayo hayakupata kibali cha Mlipaji Mkuu wa Serikali.”
Alisema tatizo la kutokusimamia kwa umakini matumizi ya Serikali lilisababisha Bajeti ya mwaka 2013/14 kuanza na deni Sh611.4 bilioni, ambazo ni matumizi ya mwaka wa fedha 2012/13 na kwamba deni hilo halikuingizwa kwenye bajeti ya 2013/14... “Hali hii inatarajiwa pia kujitokeza tena kwa kiwango kikubwa zaidi kwenye bajeti ya mwaka 2014/15. 

Malimbikizo ya madai hayo hadi Desemba 2013, yalifikia Sh2 trilioni sawa na asilimia nne ya pato la taifa. Tatizo hili ni lazima litafutiwe dawa haraka,” alisema Chenge. Alisema ongezeko la Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2014/15 kwa Sh1.605 trilioni, ikilinganishwa na Bajeti ya Serikali inayomalizika ya mwaka 2013/14 linatia shaka iwapo malengo ya ukusanyaji na matumizi yatafanikiwa.
Alisema katika mwaka wa fedha 2013/14 utekelezaji wa bajeti katika baadhi ya mafungu ulifanyika kinyume na matarajio ya Serikali, kwa maelezo kuwa yapo baadhi ya mafungu ambayo hayakutengewa fedha lakini walipewa fedha nje ya bajeti za fungu husika.

“Kwa jumla, mafungu hayo yalitumia fedha za ziada Sh115.81 bilioni sawa na asilimia 10.3 ya jumla ya fedha ambayo iliidhinishwa kwa mafungu hayo katika mwaka wa fedha 2013/14,” alisema.
Kuhusu balozi za Tanzania nje ya nchi, Chenge alisema Kamati ya Bajeti ilibaini kuwa mwaka 2012/13 zilitumia fedha zaidi ya kiwango kilichoidhinishwa na Bunge.
“Kati ya balozi 32, balozi 16 zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), zilionyesha kutumia fedha nje ya kiasi kilichoidhinishwa na Bunge ambacho ni Sh6 bilioni,” alisema.
Akichambua Bajeti ya mwaka 2014/15 ya Sh19.8 trilioni Chenge alisema: “Ukifuatilia kwa makini utaona kwamba makadirio ya makusanyo ya ndani ya Sh12.44 trilioni hayatoshi kugharimia mahitaji ya mishahara (trilioni 5.317), Deni la Taifa (trilioni 4.354) na matumizi yasiyoepukika (trilioni 3.063) ambayo kwa jumla yanatupa kiasi cha Sh12.734 trilioni. Hivyo makusanyo yetu ya ndani ya kodi ni pungufu kwa Sh0.294 trilioni.”
Alisema licha ya Serikali kutokuwa na vyanzo vya uhakika, imekopa Sh3 trilioni katika mifuko ya hifadhi ya jamii, huku ikirejesha Sh50 bilioni kila mwaka, kiasi ambacho ni kidogo na hivyo kusababisha mifuko husika kushindwa kulipa pensheni kwa wanachama wake.
Alisema Serikali ina madeni makubwa katika baadhi ya wizara zake, ikiwamo Ujenzi ambayo hujikuta ikianza mwaka mpya wa fedha na madeni ya mwaka uliopita wa fedha yanayosababishwa na kutokuwalipa makandarasi.
Alisema sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi zinazobeba asilimia 75 ya Watanzania wote, hazikui kwa kasi inayotakiwa kutokana na Serikali kutokuwekeza vya kutosha. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz
 
Vyanzo vipya vya mapato
Kambi ya Upinzani Bungeni imetaja vyanzo mbadala vya mapato ambavyo kwa mwaka vinaweza kufikia Sh6 trilioni. Akisoma maoni ya kambi hiyo, Msemaji wake kwa Wizara ya Fedha, James Mbatia alivitaja vyanzo hivyo kuwa ni kudhibiti ukwepaji wa kodi, kuongeza ufanisi Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kudhibiti misamaha hadi kufikia asilimia moja ya Pato la Taifa.
“Kuongeza ufanisi Bandari ya Dar es Salaam kwa asilimia 50 tu, pesa-fasta tozo ya asilimia 15 kwenye wakala wa kampuni za simu. Vyanzo vingine ni tozo ya asilimia moja ya manunuzi yote ya nje na tozo ya asilimia 0.5 ya mauzo yote ya nje itatengwa kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya reli,” alisema.
Alitaja vyanzo vingine ni mrabaha wa asilimia tano kwenye uvuvi wa samaki katika bahari kuu kwa meli 68 na marekebisho ya kodi sekta ya misitu. Kambi hiyo ilipendekeza maeneo mapya ya ukusanyaji wa mapato kuwa ni pamoja na sekta isiyo rasmi, wachimbaji wadogo wa madini na mapato ya kodi ya ardhi na maliasili.

Mengine ni mauzo ya mazao ya misitu, mapato ya uwindaji wa kitalii, mrabaha wa madini, taasisi za kibiashara za Serikali na mamlaka ya bandari. Alipendekeza maeneo ya kipaumbele katika bajeti yao kuwa ni utawala bora, elimu, kilimo, afya, miundombinu, nyumba na makazi. Mengine ni michezo na sanaa, ajira (kukuza uchumi vijijini) na ulinzi wa rasilimali za Taifa (wanyama, misitu, ardhi, uoto wa asili, maziwa, mito, bahari pamoja na mazao yake).

“Kambi Rasmi ya Bunge inapendekeza mishahara ya walimu iboreshwe na Serikali itoe misamaha ya kodi ya (Paye), kwenye mishahara ya walimu kama motisha ya kuwavutia wote wenye uwezo na sifa kufundisha, kuweza kufanya kazi zao kwa uadilifu.”
Akizungumzia kuhusiana na ukusanyaji wa mapato, Mbatia alisema kampuni za uwekezaji kwenye utafutaji na uchimbaji madini nchini zinapatiwa kivutio kadhaa kuendeleza shughuli zao nchini lakini kiasi kinachosamehewa kwa wawekezaji nchini huikosesha Serikali mapato ambayo ingeyapata kwa wawekezaji kwa kulipa kodi stahiki.
Nyingine ni msamaha wa mapato juu ya mtaji, wa kulipa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwa kuagiza bidhaa ndani au nje ya nchi pamoja na kampuni na makandarasi wake.
Alisema baada ya kulipa kodi ya asilimia 0.3 kampuni hizo hulipa Dola 200,000 za Marekani tu kwa mwaka bila kujali ukubwa wa shughuli za uzalishaji, faida na uchafuzi wa mazingira na madhara mengine katika jamii.
Mbatia ambaye pia ni Mbunge wa Kuteuliwa – NCCR - Mageuzi alisema kwa mujibu wa CAG, misamaha ya kodi inayotolewa kwa kampuni za uchimbaji wa madini pekee kwa mwaka 2011, ilikuwa Sh109,885 bilioni huku misamaha iliyotolewa na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), ikifikia Sh239.667 bilioni. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Na Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...