Sunday, August 04, 2013

SERIKALI: WALIOOANA NA WAHAMIAJI HARAMU WAVUNJE NDOA HIZO.....!!!

Mkuu wa mkoa wa Geita, Said Magalula

******
Serikali mkoani Geita imetoa siku saba kwa wananchi wenye ndoa na wahamiaji haramu kuvunja ndoa hizo mara moja na kurejea makwao kwa hiari.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa mkoa wa Geita, Said Magalula, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na hali ya ulinzi na usalama wa mkoa huo.

Agizo hilo limekuja siku chache, tangu Rais Jakaya Kikwete kutoa siku 14 kwa wahamiaji wote haramu kutokana nje ya nchi kuondoka kwa hiari yao kabla ya kuwasaka na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.



Katika ziara yake mkoani Kagera, Rais Kikwete alisema serikali haiwezi kuendelea kuwafumbia macho wahamiaji hao haramu kwa kuwa wamekuwa wakihatarisha amani katika mikoa ya Kagera, Kigoma na Geita kwa kujihusisha na vitendo vya ujambazi, wizi wa mifugo, migogoro ya ardhi na mauaji ya kiholela.

Aidha, amesema baada ya muda huo kuisha, operesheni kali itaanza kwa kuhusisha vyombo mbalimbali vya usalama na kwamba nguvu kubwa itaelekezwa kwenye maeneo ya visiwa, mijini, vijijini na kwenye misitu ya hifadhi ambapo hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaobainika.



Aliwatahadharisha baadhi ya viongozi wa chama na serikali wenye maslahi na wahamiaji haramu, kuwa serikali ya mkoa huo haitasita kuwakamata na kuwafikisha kortini iwapo watabainika kuwalinda wahamiaji hao haramu kwa maslahi yao binafsi.

Aliwataka wananchi kushirikiana na serikali kuwafichua watu wanaomiliki silaha kinyume cha sheria, wanaoishi na wahamiaji haramu na mawakala wao kwa kutumia namba za simu 0717 356969, 0784 518890 na 0658 376488 au ofisi yoyote ya serikali ili hatua za haraka zichukuliwe kwa lengo la kuifanya falsafa ya mkoa wa Geita ya "Amani, Umoja na Kazi" ifanikiwe. 



CHANZO: NIPASHE

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...