Monday, April 22, 2013

BI KIDUDE UMEKWENDA, UMEACHA MAJANGA YA WASANII WA KIKE BONGO!, WAJUE BAADHI YAO HAPA

Kishindo cha kuondoka kwako kwenye uso wa dunia tunayoishi kinaweza kuwa kikubwa ama kidogo au hakuna kabisa kutokana na mazingira au heshima uliyojijengea katika jamii.
Fatma Binti Baraka maarufu kwa jina la Bi Kidude aliaga dunia wiki iliyopita akiwa na zaidi ya miaka 100. Bado jina lake linatamkwa kwenye vinywa vya wengi na linaweza kuendelea kutamkwa kwa miaka mingi zaidi.
Bi Kidude, mwanamke shujaa mzaliwa wa Visiwani Zanzibar alileta mapinduzi katika muziki asilia wa mwambao. Aliitangaza Zanzibar, Tanzania na Bara la Afrika sehemu mbalimbali duniani alipokwenda kwa ziara za kimuziki. Inaaminika alifanya kazi hiyo ya muziki, mafunzo ya unyago na biashara ya hina na wanja kwa zaidi ya miaka 90. Katika kipindi chote, Bi Kidude hakushuka kimuziki hadi pale mdomo ulipoanza kuwa mzito kutokana na uzee miaka 10 kabla ya kifo chake Aprili 17, mwaka huu baada ya kuugua maradhi ya kisukari na kongosho kwa muda mrefu.
Pia inaaminika kuwa ndiye msanii mkongwe zaidi aliyekuwa akipanda jukwaani na umri mkubwa ukilinganisha na wengine unaowajua.

Shukurani kwa kazi kubwa aliyoifanya katika kukuza na kuutangaza muziki wa mwambao miaka hiyo kabla akina Zuwena Mohamed ‘Shilole’, Snura Mushi, Aisha Ramadhan ‘Isha Mashauzi’, Khadija Kopa na wengine wengi hamjazaliwa na hata baada ya kuzaliwa.
Mkumbuke kuwa matunda ya muziki mnaofanya, Bi Kidude ndiye aliyekwangua barabara.
Ngoja leo nizungumze na mastaa wa muziki wa kike Bongo. Najua mpo wachache lakini kati yenu hakuna anayeweza kupiga kifua kuwa amesaidia kukuza muziki wa kizazi kipya kama alivyofanya legendary Bi Kidude katika muziki asilia wa mwambao.
Wengi wenu mmeishia njiani mapema. Hii ni kwa sababu msingi mliouweka haukuwa imara na hata kama mlikuwa na malengo, basi mlishindwa kuyapigania.
Historia ya Bi Kidude inatutoa huko kwenye kukata tamaa mapema, ama kwa kukutana na vigingi vingi tukashindwa kuvivuka au kwa kupenda zaidi starehe na kusahahu kazi.
Wapo akina Ray C, Sister P, Rah P, Zay B na hata akina Maunda Zorro, Besta, K-lyn na wengine wengi. Labda Mwasiti na Lady Jaydee ambaye ameamka usingizini na kuanza harakati za kuupigania muziki huo.
Mnaonaje mipango mliyojiwekea akina Linah, Recho, Dyna, Vanessa na wengine? Je, mtafikia kiwango cha Bi Kidude ambaye asilimia 90 na ushee ya maisha yake aliitumia katika muziki?
Nawajua baadhi yenu ambao mmeingia kwenye muziki na sanaa nyingine kwa malengo tofauti. Hebu ona wakongwe wa kike kwenye Bongo Fleva wako wapi?
Wale tuliowasikia kitambo wakicheza kihasara majukwaani walionekana na wanaume wakaolewa na kuachana na muziki. Unajua kwa nini? Hamkuwa na lengo la kuukuza na kuuendeleza muziki huo. Mlikuwa mnataka wanaume na mkapata kama wanavyofanya wenzenu kwenye tasnia ya filamu.
Kwa taarifa yenu jamii imewashtukia, haitaki kuwasikia kwa kuona kuwa ninyi ni wazugaji au wazinguaji. Badilikeni. Jipangeni kama kweli mnataka kuweka heshima kama ya Bi Kidude.
Ulevi wa aina zote kuanzia pombe hadi unga, ufuska au umalaya, tamaa mbaya, dharau, majungu, fitina, kujigawa makundi na mengine yanayofanana na hayo yatawaangusha tu, mtabaki kulalamikia kubaniwa na kuombwa rushwa ya ngono jambo ambalo si kweli. Heshima ni jinsi unavyojiweka. Kwa heri Bi Kidude lakini wasanii wa kike Bongo wasipobadilika na kujitambua ni majanga tupu. For the of game!

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...