Sunday, March 03, 2013

TFF YAIKOMALIA SERIKALI

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limesema ipo haja kwa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara kufikiria upya uamuzi wake wa kutengua usajili wa Katiba ya TFF ya mwaka 2012 na kutaka itumike ya mwaka 2006, kwani hautekelezeki.

Akizungumza na waandishi wa habari leo mchana, mara baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji, Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema ni muhimu jambo hilo likaangaliwa upya kwa sababu athari zake ni mbaya, na pengine Dk. Mukangara hakushauriwa vizuri kabla ya kufanya uamuzi huo.

“Kamati ya Utendaji ya TFF haitaki kubishana na Mheshimiwa Waziri hata kidogo, ila tunaamini wakati anatamka haya hakufahamu madhara yake, athari zake na ugumu wa utekelezaji wake. Kwa waliomshauri hili, wamemshauri vibaya,” amesema Rais Tenga.

Amesema rai ya TFF kwa Waziri ni kuwaita ili wamweleze ni kitu gani wafanye kunusuru mpira wa miguu wa Tanzania, kwani wanaamini jambo hili litakwisha baada ya kumwelimisha hasa kutokana na ukweli kuwa kabla ya kufanya uamuzi huo hakuwasikiliza.

Katika mkutano huo, Rais Tenga alianza kwa kusema kuwa TFF inaiheshimu sana Serikali, hivyo inaheshimu maagizo yaliyotolewa na Waziri, lakini akaongeza kuwa TFF ina wajibu wa kutoa ufafanuzi juu ya maagizo hayo.

Amesema lengo la kuelezea historia ya TFF ilikotoka ni kubaini migongano ya maagizo hayo na taratibu za TFF ambazo kwa bahati mbaya zinasigana na maagizo hayo.

Rais Tenga amesema TFF ni chombo cha wanachama, ambapo wanachama wake ni vyama vya mikoa, vyama shiriki na klabu za Ligi Kuu, na ina taratibu za kufanya uamuzi kwa mujibu wa Katiba yake na za wanachama wake ambazo zimeidhinishwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Amesema si TFF pekee, bali vyama vya nchi zote ambavyo vimeunganishwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), zinaheshimu na kufuata maagizo na miongozi ya shirikisho hilo la kimataifa la mpira wa miguu.

Rais Tenga amesema TFF haitakiwi kuingiliwa katika uongozi na uendeshaji wake, kwani jambo hilo likitokea rungu la FIFA litaiangukia TFF, na madhara yake ni makubwa. Miongozo ya FIFA inasisitiza uhuru wa wanachama wake katika uendeshaji shughuli za mpira wa miguu, na iko kwenye Katiba ya TFF.

“Sheria za nchi ndizo zilizozaa Katiba ya TFF. TFF ni chama kamili kinatakiwa kufanya uamuzi wake ili mradi uzingatie madhumuni ya kuanzishwa kwake. Leo TFF ikiacha mpira wa miguu na kuanza kujishughulisha na gofu, hapo Msajili ana haki ya kuingilia,” amesema Rais Tenga.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...