Jana, Bingwa wa Dunia wa uzani wa kati (super middle), unaotambuliwa na Shirikisho la Ngumi Duniani (WBF), Francis Cheka alitembelea Bunge baada ya kutwaa taji hilo karibuni na jana hiyohiyo, Bunge hilo lilishuhudia ngumi kavukavu katika vurugu kubwa pengine kuliko zote zilizowahi kutokea katika ukumbi wake.Katika masumbwi hayo yasiyo rasmi, Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi 'Sugu' anadaiwa kumpiga kichwa Askari wa Bunge na kumchania sare na kung'oa kipaza sauti.
Mbilinyi jana alisema alikuwa
anatafutwa na polisi huku akisema hilo limemshangaza akidai kwamba yeye
ndiye aliyeshambuliwa na askari huyo.
Vurugu hizo zilitokea baada ya Naibu
Spika, Job Ndugai kuamuru kutolewa nje kwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya
Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe.
Katika vurugu hizo Mbilinyi alibebwa juujuu na polisi hadi nje ya ukumbi huku akiwa hana viatu.
Pamoja na tafrani hiyo, Ndugai alisema
wakati akihitimisha kikao cha Bunge kipindi cha asubuhi kuwa
amewasamehe wabunge wote waliohusika na kosa hilo la utovu wa nidhamu na
kuwaruhusu kurejea kipindi cha jioni kuendelea na Muswada wa
Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Hata hivyo, wabunge wote
CUF, NCCR-Mageuzi na Chadema ambao baada ya tukio hilo walitoka nje ya
ukumbi, hawakurejea na baadaye walitoa msimamo wa pamoja wakisema
hawatashiriki katika mjadala huo.