Tuesday, September 03, 2013

RWANDA YAONGEZA USHURU KWA MIZIGO IPITAYO BADARI YA DAR TU

paul kagame 2d247
NI dhahiri sasa biashara ya kupitisha mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam, imekuwa moto, baada ya Serikali ya Rwanda kupandisha tozo ya ushuru kutoka dola za Marekani 152 hadi 500 ambazo ni sawa na Sh 800, 000 za Tanzania.
Hali hii inawezekana kwa namna moja au nyingine, imetokana na mzozo kati ya Rais Jakaya Kikwete na Rais Paul Kagame wa Rwanda, ambao umepelekea wafanyabiashara wa Rwanda na Uganda kutishia kuacha kupitisha mizigo yao katika Bandari ya Dar es Salaam.


Itakumbukwa mzozo huo, umekuja baada ya Rais Kikwete kumshauri Rais Kagame akubali kukutana na waasi wanaoendelea na vita mashariki mwa nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), lakini ushauri huo unaonekana kupokelewa tofauti na Rais Kagame.
Siri ya kupandishwa kwa gharama hizo, imefichuka jana baada ya malori mengi ya wafanyabiashara wa Tanzania kukwama katika mpaka wa Rusumo mkoani Kagera.

Itakumbukwa hatua hii, imekuja wiki chache baada ya Chama cha Wasafirishaji wa Mafuta Tanzania (TATOA), kuitahadharisha Serikali kuwa Rwanda na Uganda, zimeazimia kwa pamoja kuacha kupitisha mizigo yao kwenye Bandari ya Dar es Salaam kuanzia Septemba mosi.

Awali, mamlaka mbalimbali za Serikali mjini Dar es Salaam, zilidai hakuna uwezekano wa nchi hizo mbili wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kuacha kuitumia Bandari ya Dar es Salaam zikidai kuwa hizo ni dhana tu.
Lakini taarifa zilizolifikia MTANZANIA jana asubuhi kutoka Rusumo, mpakani mwa Rwanda na Tanzania, zinasema katika kile kinachoonekana kuwa ni dhamira ya dhati ya kuachana na matumizi ya bandari na barabara za Tanzania, Mamlaka ya Mapato ya Rwanda (RRA), imepandisha ghafla tozo la barabara na kusababisha usumbufu mkubwa mpakani.

Chanzo chetu cha habari kutoka Rusumo, kilisema RRA imepandisha tozo hilo maarufu kama 'Road Toll' kutoka Dola za Marekani 152 hadi Dola 500 (sawa na Sh 800,000), ikiwa ni ongezeko la zaidi ya asilimia 200.
"Hali ni mbaya sana hapa mpakani Rusumo, kwani tangu jana (juzi, Jumapili), tumekwama hatujui la kufanya baada ya Rwanda kuongeza 'Road Toll' kwa kiwango kikubwa.

"Foleni ya magari sasa imeziba kabisa barabara kuanzia Rusumo hadi Benaco na pia kuelekea barabara nyingine ya kwenda Ngara. Sijui itakuwaje, nadhani ni lazima kulipa ongezeko hili.
"Kinachostaajabisha na kudhihirisha wazi kuwa hawa jamaa (Rwanda) sasa hawatutaki ni kwamba, magari ya namba za Kenya, yanalipa Dola 152 kama kawaida na kuendelea na safari," mmoja wa madereva wa magari ya mizigo, Maneno Kagasha, alimkariri dereva mwenzake aliyeko mpakani.

Alisema magari mengi yaliyokwama Rusumo, yamebeba bidhaa tofauti kupeleka mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), katika miji ya Bukavu na Goma iliyo umbali wa kilomita kati ya 300 na 450 kutoka Rusumo.
Hatua ya RRA kupandisha Road Toll kwa kiwango kikubwa, inaonekana machoni mwa wadadisi wa mambo kama njia mojawapo ya kuonyesha hasira za Serikali ya Rwanda chini ya Rais Paul Kagame dhidi ya Tanzania.

MTANZANIA liliwasiliana na mamlaka za Serikali kuhusu hilo na kuombwa kupewa muda wa kuwasiliana na watu wa mpakani kuangalia kwa kina suala hilo.
"Hizi Road Toll kwa nchi za jumuiya yetu zipo, lakini kupandisha kwa kiwango kikubwa namna hii, hili ni suala jingine. Hakika ni suala kubwa," alisema ofisa mmoja wa TCCIA bila kupenda kutajwa gazetini.

Uhusiano wa Rwanda na Tanzania kwa muda sasa, umekuwa legelege na huenda hatua hii ya sasa ni ya kutaka kuzuia magari ya Tanzania yasipeleke bidhaa huko Goma ambako vita vinaendelea kati ya waasi wa M23 wanaoungwa mkono na Rwanda na majeshi ya RDC, yakishirikiana na ya Umoja wa Mataifa yanayoundwa na bataliani moja ya Tanzania.RC Kagera

Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali Fabian Masawe, alipoulizwa kuhusiana na magari hayo kukwama, alisema hana taarifa kwa sababu muda huo alikuwa safari kutoka Ngara kwenda Bukoba mjini.

"Nipe muda kidogo, nipo njiani natoka Ngara naelekea mjini, naanza kulifuatilia suala hili haraka ili kujua ukweli, nitakujulisha," alisema Kanali mstaafu Masawe.
Juzi wasomi na wanasiasa mbalimbali, walisema Bandari ya Dar es Salaam ina matatizo mengi ambayo yanapaswa kutatuliwa ili kurudisha imani kwa watumiaji.

:CHANZO MTANZAIA

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...