Wednesday, March 18, 2015

'KURA YA MAONI IPO PALE PALE'

Kaimu kiongozi wa shughuli za serikali bungeni Mh. Samuel Sitta.
SERIKALI imesema haiwezi kubadili msimamo wake kuhusu upigaji wa Kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa, licha ya kuwepo maoni ya viongozi wa dini ambao wanataka jambo hilo lisitishwe.

Kaimu Kiongozi wa shughuli za Serikali bungeni, Samuel Sitta alisema jana mjini hapa kuwa pamoja na kuwepo kwa tofauti kati ya Jukwaa la Wakristo na Kiongozi wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, msimamo wa Serikali uko pale pale.

Sitta, ambaye anakaimu shughuli za serikali bungeni kutokana na kutokuwepo kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, alisema Serikali inakubaliana na maoni ya Kardinali Pengo kuwa waumini waachwe waamue wenyewe kuhusu Katiba Inayopendekezwa.

Alisema kama viongozi wa dini wamegawanyika hakuna namna ya kuwafanya wawe na kauli moja, lakini akasisitiza kuwa jambo la msingi ni kuachwa kwa mtu aamue mwenyewe aina ya kura atakayopiga.

Hivi karibuni Pengo alitofautiana na Baraza la Maaskofu (TEC) na Jukwaa la Wakristo ambao wanataka upigaji wa kura ya maoni usitishwe, kwa maelezo kuwa wananchi hawajapewa muda wa kuisoma na kuielewa katiba hiyo na kama Serikali itang’ang’ania ni vyema waumini wa kanisa wapige kura ya hapana. Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.


Sitta, ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Kutunga Katiba (BMK) alisema Serikali haiwezi kuwakadiria waseme nini au mambo yao yaishe vipi. “Demokrasia yoyote huwa na mawazo ambayo yanatofautiana. Msimamo wa serikali ni ule ule kwamba tutaendelea mpaka kupiga kura ya maoni,” alisema Sitta.

Mwanasiasa huyo mkongwe alisema; “Wananchi wataamua wenyewe na wale watakaoona kwamba wameshawishiwa na wakuu wao wa dini kufuata hilo tamko hawawezi kuwazuia na wale watakaoona kuwa hakuna suala la imani ni utashi wa kisiasa nao watakuwa na msimamo wao.”

Sitta alisisitiza kuwa ratiba ya Serikali haibadilishwi na tofauti ya kimtizamo kutoka kwa viongozi hao na kwamba Kura ya Maoni itapigwa Aprili 30 kama ilivyopangwa.

Mvutano ulioibuka hivi karibuni kati ya Kadinali Pengo na viongozi wengine wa madhehebu ya Kikristo, umeibua mjadala mzito kwenye jamii huku wengine wakieleza kuwa viongozi hao wanawayumbisha wananchi.

Kauli ya Pengo imekuja huku tayari tamko ambalo lilitolewa na TEC limesambazwa makanisani na tayari lilishasomwa katika baadhi ya parokia na vigango.

Msimamo wa Kadinali Pengo ni kwamba wananchi waisome na waielewe Katiba hiyo, kwani ndiyo wajibu wa msingi ambao Wakristo wanao kwa sasa ili kupiga kura inayostahili wakati ukifika.

Kuhusu agizo la waumini kuikataa Katiba Inayopendekezwa, Kadinali Pengo katika maoni yake anaeleza kuwa wao wakiwa viongozi wa watu, hawana mamlaka wala uwezo huo, bali wenye uwezo ni wananchi wenyewe.

Hata hivyo, Kadinali Pengo alitaka tamko hilo lisambazwe kwenye parokia na vigango vyote vya Jimbo Kuu la Dar es Salaam ili waumini wasomewe, wauelewe kwanza, ili hatimaye waweze kufanya uamuzi sahihi wakielewa ni nini wanachokitakiwa kukifanya.
Jukwaa la Wakristo linaundwa na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT). Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...