Thursday, January 01, 2015

MWAKYEMBE AFUKUZA KAZI VIGOGO 6 WA RELI

Dk Harison Mwakyembe.
 Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe

Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe ameagiza wafanyakazi sita wa Shirika la Reli Tanzania (TRL), wafukuzwe kazi na polisi wawakamate na kuwalaza rumande kuanzia jana kutokana na tuhuma za wizi.
Pia, ameagiza mali za watuhumiwa hao, zichunguzwe na ikibainika ni zaidi ya kipato chao cha kawaida, zipigwe mnada na Bodi ya Wakurugenzi ikae na kuangalia hatua zaidi za kuchukua.
Dk Mwakyembe alitoa maamuzi hayo jana baada ya kuzungumza na wafanyakazi wa TRL na kuonekana kutoridhishwa na vitendo vya wizi, vinavyoendelea katika shirika hilo.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Stanley Makunja, Stanley Andrew, Edward Benedicto, Lucy Mtinya, B. Ruoga na Jackson Moses.
Hata hivyo, Mwakyembe alipoombwa na waandishi wa habari, kufafanua vituo vya kazi vya watuhumiwa hao, alidai kwamba wote ni wa TRL na wamewajibishwa kama wafanyakazi wa TRL. Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.

Pia, alisema anayo madai na tuhuma nyingi zaidi ya hizo, lakini hajayahakiki vizuri na anaendelea kuyafanyia uchunguzi na utakapokamilika atachukua hatua kali zaidi.
“Tumekuwa tukifanya jitihada nyingi sana kuhakikisha TRL ukiwemo kutoa upendeleo katika bajeti, lakini bado tunakwama kutokana na vitendo vya wizi vinavyoendelea... watu wanasimamisha treni wanaiba mpaka mafuta bila hata woga,” alisema.
Alisema, “nimewabembeleza kwa muda mrefu, nimechoka, mara nyingi nawaambia na kusisitiza wafanye kazi kwa uadilifu na wasiibe, lakini hawasikii hivyo nimeamua kuchukua hatua hizi kwa kuanzia”.
Akitoa mfano, Dk Mwakyembe alisema kuwa miongoni mwa wizi uliofanyika ni wizi wa fedha, zinazotozwa katika tiketi za abiria wa treni, ambapo abiria hutozwa hela halali ya juu, lakini kinachoingizwa katika kopi inayobaki TRL ni kiasi kidogo, hata robo ya fedha halisi haifiki.
Alisema wafanyakazi hao wamekuwa wanakatisha tiketi na kuweka ganda gumu chini hivyo kiasi kile hakiingii na baadaye huandika kiasi cha fedha wanachotaka.
Alisema baadhi ya tiketi alizofanyia uchunguzi, kuna tiketi moja ya Sh 61,200 ambayo mteja alipewa na kuilipia, lakini fedha iliyoingia kwenye kopi ya TRL ni Sh 16,200. “Nasema waliofanya hivi wakamatwe na watiwe rumande mara moja.
Tiketi nyingine ni ya Sh 50,200 ambayo mteja alipewa na kuilipia, lakini TRL imeandikwa Sh 13,200,” alisema. Alisema “tiketi nyingine ya Sh 74,200 mteja aliilipia na kopi yake iliyoingia TRL inaonesha ni Sh 13,600 na nyingine ya Sh 57,600 lakini iliyoingia TRL ni Sh 6,700 tu, halafu mimi nikae kushindana na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya kumwambia aongeze mishahara wakati hela mnachukua”.
Aidha, Mwakyembe alisema kuwa Tume imeundwa kukagua mabehewa ya mizigo, yanayoingizwa na kampuni ya India ya Hindustan Engineering and Industries Ltd (HEIL), yanayodaiwa kwamba yana hitilafu na hivyo kusababisha ajali.
“Nimemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara kuungana na timu ya wataalamu wanne kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, TRL, Bodi ya Wakandarasi na Sumatra kuchunguza mabehewa yaliyodondoka na mizigo hivi karibuni, pia timu hiyo itakwenda India yanapotoka mabehewa kwenda kujiridhisha kama kuna dosari, basi tutasitisha mabehewa yaliyosalia yasiletwe nchini na wahusika watachukuliwa hatua,” alisema.
Hata hivyo, pamoja na hatua hizo alizochukua Dk Mwakyembe, baadhi ya wafanyakazi wa shirika hilo walionekana kutoridhika nazo kwa madai kwamba waliofanya ufisadi mkubwa, wakiwemo viongozi waandamizi, wameachwa na kuchukuliwa hatua wenzao.
Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli Tanzania (TRAWU), Erasto Kiwele alisema maamuzi aliyochukua Dk Mwakyembe ni maamuzi mepesi, kwa sababu wapo watu walioleta mabehewa mabovu, wao wameachwa na hawajakamatwa wala kufukuzwa kazi, isipokuwa wanaofukuzwa ni wanaoiba mafuta.
“Maamuzi haya ni mepesi sana na hatukuyatarajia, kwa sababu wameachwa wanaoiba mabilioni na walioingiza mabehewa mabovu yanayodondoka na kupata ajali kila mara, pia wameachwa viongozi waandamizi wanaofanya ufisadi wa kukodisha kiberenge kwa Sh 10,000 kwa mwezi, lakini wamechukuliwa hao wanaofanya wizi mdogo, tunajua wote wizi sio jambo jema na hatusemi wangepaswa kuachwa, ila ilitakiwa wachukuliwe hatua wote, maamuzi haya ni mepesi sana” alisema. Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.

Na Habari Leo

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...