Thursday, September 11, 2014

YONA AANZA KUJITETEA KISUTU



Waziri wa zamani wa Wizara ya Nishati na Madini, Daniel Yona. Picha na Maktaba 

Waziri wa zamani wa Wizara ya Nishati na Madini, Daniel Yona ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa mchakato wa kumpata mkaguzi wa madini ya dhahabu ulifuata utaratibu kwa kusimamiwa na Gavana wa Benki Kuu Tanzania (BoT).

Aliyaeleza hayo jana alipojitetea dhidi ya mashtaka ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia Serikali hasara ya Sh11.7 bilioni yanayomkabili na wenzake wawili.

Akiongozwa na wakili wake, Eliasa Msuya kutoa ushahidi wa utetezi mbele ya jopo la mahakimu watatu wanaoisikiliza kesi hiyo, John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela, Yona alidai kuwa wakati wakiendelea na utaratibu wa kumtafuta mkaguzi wa dhahabu walipata ushauri kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).

Alidai kuwa utaratibu wa kumtafuta mkaguzi huyo nchini ulitokana na malalamiko ya wananchi, Bunge, vyombo vya habari na mashirika yasiyo ya kiserikali mwaka 2002, kuhusu mapato ya madini hayo yaliyokuwa yakichimbwa na kampuni tano za kigeni. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

“Wizara ya Nishati iliamua kuhakiki gharama za madini hayo kwa kuwa BoT ndiyo iliyosimamia akaunti za kampuni hizo ndani na nje ya nchi, iliruhusu kufungua akaunti zake pamoja, tulikubaliana kumtafuta mkaguzi wa dhahabu,” alieleza Yona.

Yona alidai kuwa BoT na wizara, walianza mchakato huo wa kuhakikisha anapatikana mzabuni mkaguzi wa dhahabu kwa kufuata utaratibu na sheria za nchi.

Alidai kuwa baada ya kufanyika kwa majadiliano, Mei 11, 2003 aliamwandikia dokezo Rais wa wakati huo, Benjamin Mkapa kuhusu ukaguzi wa dhahabu.

Akiendelea kujitetea, Yona alidai kuwa alimfahamisha Rais Mkapa kuhusu majadiliano waliyoyafanya kati ya Wizara ya Nishati, Wizara ya Fedha, BoT na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwa yanaendelea vizuri.

Aliongeza kuwa Machi 3, 2003, alimwandikia Rais dokezo kuomba aruhusu kutekeleza ukaguzi wa dhahabu kwa kufuata taratibu na sheria.

Yona alidai kuwa Machi 20, 2003 Rais alimjibu kwamba anakubali waendelee na mchakato haraka na kwamba wao walimwahidi kuwa mchakato huo utazingatia mapato ya nchi na ushauri wa AG na kwamba walizingatia hilo.

Hata hivyo, Yona hakuweza kuendelea kutoa ushahidi wake wa utetezi baada ya Wakili wa Serikali, Oswald Tibabyekomya kupinga kupokewa kwa nyaraka ya kielelezo cha ushahidi kutoka Ofisi ya AG.

Baada ya kutolewa kwa hoja hiyo, mahakimu hao walikubaliana kuiahirisha kesi hiyo hadi leo kwa ajili ya kumpa nafasi wakili wa serikali, Oswald kujiridhisha na kielelezo hicho.
Washtakiwa katika kesi hiyo ni waziri wa zamani wa Fedha, Basil Mramba, Yona na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja.
Washtakiwa hao wanakabiliwa mashtaka ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia Serikali hasara ya Sh11.7 bilioni.
Inadaiwa kwamba walitenda makosa hayo Agosti, 2002 kwa kuisamehe kodi Kampuni ya Ukaguzi wa Madini ya Alex Stewart ya nchini Uingereza kinyume cha sheria. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...