Friday, December 13, 2013

ZITTO AWASHA MOTO MPYA CHADEMA...!!!



Siku moja baada ya kuwasilisha maelezo yake ya utetezi baada ya kuvuliwa nyadhifa zake ndani ya Chadema, aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe amekata rufaa Baraza Kuu kupinga hatua hiyo.


Zitto pamoja na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba na Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk Kitila Mkumbo walivuliwa nyadhifa zao na Kikao cha Kamati Kuu kilichofanyika Novemba 20 na 21 jijini Dar es Salaam.


Akizungumza jana, Mwanasheria wa Zitto, Albert Msando alitaja sababu mbili za kukata rufaa kuwa ni kukiukwa kwa taratibu za kuchukua hatua za nidhamu na sababu zilizotolewa kutokuwa sahihi.


Hata hivyo, Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika alisema mambo hayo yalishatolewa ufafanuzi na chama na kwamba kukata rufaa ni haki ya kikatiba kwa mwanachama yeyote.


“Kukata rufaa ni haki ya kikatiba ya wanachama yeyote. Rufaa ikatwe tu, itashughulikiwa kwa mujibu wa katiba, kanuni, maadili na itifaki ya chama. Hata hivyo, ieleweke, rufani inahusu kuvuliwa nafasi za uongozi, kusudio hilo haliwaondolei wajibu wa kujieleza kwa maandishi mbele ya Kamati Kuu kwa nini wasifukuzwe uanachama,” alisema Mnyika.


Sababu za kukata rufaa


Akifafanua sababu za kukata rufaa, Msando alitaja kifungu cha 6.5.6 cha Kanuni ya Uendeshaji ya chama hicho, akisema utaratibu uliotakiwa kufuatwa kabla ya kumchukulia hatua za kinidhamu kiongozi kwa mujibu wa Katiba na Kanuni ni kupewa kwanza mashtaka kwa maandishi ili apate nafasi ya kujibu.


“Kiongozi yeyote hatachukuliwa hatua za kinidhamu bila kwanza kupewa mashtaka yake kwa maandishi na mamlaka husika na kupewa nafasi ya kujibu mashtaka kwa maandishi,” alisema na kuongeza:


“Kwa mujibu wa ibara ya 5.4.3 na 5.4.4 ya Katiba mwanachama yeyote hatachukuliwa hatua za kinidhamu ama kuonywa ama kuachishwa ama kufukuzwa uanachama bila kujulishwa makosa yake kwa maandishi na kutakiwa kutoa majibu katika muda usiopungua wiki mbili.”


Alitaja vipengele vingine ni kupewa nafasi ya kujitetea mbele ya kikao kinachohusika na atajulishwa kwa maandishi uamuzi wa kikao ndani ya wiki mbili baada ya kusikilizwa.


Hata hivyo, kipengele ‘d’ kinasema: “Kamati Kuu inaweza kuchukua hatua za dharura bila kuzingatia utaratibu (b), (c) hapo juu kama itaona masilahi ya chama kwa ujumla yanaweza kuathiriwa isipokuwa mwanachama au kiongozi anayelalamikiwa atalazimika kuitwa kwenye kikao husika.


Alifafanua kuwa, siku ya kikao cha Kamati Kuu, Zitto hakupewa mashtaka yake bali aliyakuta ndani ya kikao baada ya kupewa taarifa kwa ujumbe wa simu (text message au sms). Zitto hakuwepo katika mkutano wa jana na waandishi wa habari.
Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...