Friday, December 13, 2013

AZIMIO LA KUWANG'OA MAWAZIRI LAPITISHWA RASMI NA BUNGE...!!!


Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia.
********
Bunge limepitisha azimio la kuwataka mawaziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), kujipima iwapo wanatosha kuendelea kuongoza wizara hiyo nyeti.
Azimio hilo lilipitishwa jana na wabunge kwa kura ya ndiyo bila kupingwa, baada ya kuhojiwa na Spika wa Bunge Anne Makinda iwapo wanaipokea taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (Laac) iliyowasilishwa na Mwenyekiti wake Rajabu Mbaruku.
Moja ya mapendekezo yake ni Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia na manaibu wake, Aggrey Mwanri na Kassim Majaliwa kujipima kama wanatosha kuendelea kuongoza wizara hiyo kutokana na kugubikwa na vitendo vya ufisadi.
Kwa mujibu wa taratibu za Bunge, taarifa ya kamati inapowasilishwa na kupitishwa pamoja na mapendekezo yake, huwa ni azimio kamili ambapo Serikali hutakiwa kutoa maelezo ya utekelezaji wake.
Kabla ya azimio hilo kupitishwa, Mwenyekiti wa Laac, Rajabu Mbaruku alijibu michango ya wabunge waliochangia katika taarifa ya kamati yake iliyowasilishwa Ijumaa iliyopita, akiwemo Waziri Ghasia.
Akizungumza baadaye, Mbaruku alisema hayo ndiyo mapendekezo na Serikali itatakiwa kuyatolea maelezo ya jinsi yatakavyotekelezwa. “Hata waziri mkuu nimemtaja kwa jina, na nimesisitiza kama ananisikia kuhusu ofisi yake,” alisema.
Katika mchango wake, Waziri Ghasia alijaribu kupangua tuhuma mbalimbali zilizoelekezwa katika wizara yake ikiwamo kuwapo ufisadi, ubadhirifu na mtandao wa wizi unaohusisha Hazina, Wizara na Halmashauri.
Ghasia alikiri Halmashauri ya Mbarali ilitumiwa fedha kuliko kiwango kilichoidhinishwa na Bunge na kwamba
suala la halmashauri mbili za Tanga kupewa zaidi ya Sh2 bilioni haikuwa sahihi bali yalikuwa ni makosa ya Mkaguzi Mkuu wa Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG).
Kuhusu ufisadi wa zaidi ya Sh600 milioni zilizotolewa na wafadhili kwa ajili ya mpango wa maboresho ya Serikali za Mitaa, alisema haamini kama maneno yaliyonukuliwa na vyombo vya habari kuhusu fedha hizo yalisemwa na wafadhili.
Wafadhili wa mradi huo walinukuliwa wakilalamikia ufisadi huo na kudai kwa sasa hawana la kufanya na wanamwachia Rais, huku wakieleza kushangazwa na Rais kuteua watu dhaifu kuendesha wizara nyeti kama Tamisemi.
Kuhusu hilo, Ghasia alisema hadhani maneno hayo ni ya wafadhili akisema ni majungu, ni maneno ya waandishi kwa sababu huwa wanatafuta mambo yanayogusa jambo fulani ili kuuza magazeti.
MWANANCHI

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...