Thursday, April 04, 2013

Chadema wamtuhumu Mwakyembe kutoa zabuni kinyume cha sheria

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimemtuhumu Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe kwamba alitoa zabuni ya ujenzi wa bandari ya nchikavu kwa kampuni inayomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), kinyume cha sheria za ununuzi. Chadema walisema jana kwamba, kampuni hiyo ni Jitegemee Trading Company ambayo ilipewa zabuni ya ujenzi wa bandari katika Viwanja vya Sukita pasipokuwa na mchakato wa kushindanisha kampuni nyingine. 
Mkurugenzi wa Oganaizesheni na Mafunzo wa Chadema, Benson Kigaila alisema: “Mwakyembe aseme alitoa zabuni hiyo kwa Jitegemee kwa kuzingatia vigezo gani? Kampuni ngapi zilishindanishwa katika mchakato huo na asipofanya hivyo hastahili kukaa wizarani hapo bali alipelekwa Segerea gerezani kwani ni kosa kubwa kutoa zabuni kinyemela.”
Hata hivyo, Dk Mwakyembe, ambaye yuko jimboni kwake Kyela mkoani Mbeya alipoulizwa kuhusu madai hayo alijibu na kukata simu; “Mimi nina kazi ya kuongoza wizara na wao Chadema wana kazi ya kuchonga mdomo, hivyo waache mimi niongoze Serikali.
Kigaila alituhumu mradi huo ulitakiwa kujengwa ndani ya Halmashauri ya Temeke, lakini katika hali ya kushangaza CCM waliamua kuhamishia Bonde la Msimbazi.
“Kampuni hiyo tayari imetengewa Sh10 bilioni katika bajeti ya 2013/14 itakayosomwa bungeni, itakuaje Serikali inawafukuza watu kuishi mabondeni, lakini wao wanapeleka mradi huo bondeni?
“Hizo zote ni njama za CCM kujikusanyia fedha kwa ajili ya kampeni za uchaguzi wa 2015,” alisema Kigaila.
Kigaila alidai kumshangaa Dk Mwakyembe kwa kubadilika na kutoa zabuni kwa kampuni, ambayo haijafanyiwa upembuzi yakinifu wakati waziri huyo aliwahi kuibeza Kampuni ya Kufua Umeme ya Richmond wakati akiwa Mwenyekiti wa Kamati Teule ya Bunge 2007.
“Mnakumbuka Dk Mwakyembe alidai Richmond haikufanyiwa upembuzi yakinifu na kutaka ipokonywe tenda, kwa nini leo hii anatoa zabuni kwa kampuni ya chama chake bila kuitangaza?”alihoji.
Alipotafutwa Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye, alisema CCM watafuatilia ukweli wa jambo hilo. “Nipe muda nifuatilie huko Jitegemee ili kujua tenda ilivyotolewa ilikwenda wapi,” alisema Nape.
Naye Meneja wa Kampuni ya Jitegemee, Esther Nyawazwa alisema wizara ilileta maombi ofisini kwao na baada ya hapo mawasiliano yaliendelea kupitia kwa Mwenyekiti wa Bodi, Peter Machunde.
“Wizara ilileta `application’ (maombi) ya zabuni ofisini kwetu ya kuomba kujenga mradi wa kituo pale kwenye Bonde la Msimbazi na baada ya hapo mawasiliano yaliendelea kati ya wizara na mwenyekiti wa bodi, kwa hiyo sasa sifahamu maendeleo ya mradi,” alisema Nyawazwa na kuongeza:“Mimi jukumu langu ni kutekeleza niliyoagizwa, hivyo ninashauri uwasiliane na mwenyekiti wa bodi kwa ufafanuzi zaidi.” Alipotafutwa kupitia simu yake ya kiganjani, Machunde hakupatikana kwani ilikuwa ikiita bila kupokewa.     
Habari na Ibrahim Yamola, Mwananchi
Chanzo - Mtanzania

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...