Monday, October 23, 2017

USHAHIDI ALIOUTOA LULU MAHAKAMANI KUHUSU KIFO CHA KANUMBA

Msanii wa filamu, Elizabeth Michael (22) amejitetea katika kesi ya kuuwa bila kukusudia katika Mahakama Kuu ya Tanzania.

Katika utetezi wake, Lulu amesema anakumbuka siku ya tukio ilikuwa Ijumaa ya April 6, 2012 ambapo aliahidiana na rafiki zake kwamba wangetoka usiku.

Amesema kuwa asubuhi ya siku hiyo alienda kuonana na rafiki zake maeneo ya Mikocheni, ambapo pia alikuwa akiwasiliana na Kanumba.

"Marehemu alikuwa ni msanii mwenzangu lakini pia nilikuwa naye na mahusiano naye ya kimapenzi,".

Lulu alisema kuwa marehemu Kanumba alikuwa hapendi kumuona akitoka, hivyo hadi siku ya tukio hakutaka kumwambia kwamba atatoka na rafiki zake.


"Hata hivyo ilipofika saa 6 kasoro usiku, nilimpigia simu Kanumba na kumwambia nataka nitoke na rafiki zangu, hivyo nitapitia nyumbani kwake nimuage,".

Lulu amesema alienda hadi nyumbani kwa marehemu, ambapo ni Sinza Vatican na akamwambia akikaribia atampigia simu.

"Nilipompigia tena simu akanambia anataka kwenda kuoga, hivyo kama nikifika nipitilize hadi chumbani maana hataweza kupokea simu, ".

Lulu amesema kuwa alipofika nyumbani aliingia mpaka chumbani, ambapo alimkuta Kanumba akiwa kwenye dressing table akipaka mafuta kwenye nywele, huku akiwa anakunywa pombe aina ya Jack Daniel.

Amesema kuwa kutokana na chumba hicho kutokuwa na sehemu ya kukaa, aliamua kukaa kitandani huku akisalimiana na marehemu.

"Baada ya muda kidogo simu ya Kanumba ikaita ambapo alikuwa akiongea na Charles Baba akimuuliza kama ataenda kwenye muziki wa bendi usiku huo, ambapo Kanumba alimwambia anamalizia kujiandaa anakuja,ambapo na mimi nikamwambia nataka nitoke na rafiki zangu,".

Lulu amesema kuwa baada ya kumwambia Kanumba kuwa anataka kutoka alianza kuumuliza anataka kwenda wapi.

"Nilimjibu kuwa nataka nitoke na rafiki zangu twende Disco mimi sipendi muziki wa Dansi kwani nj kama wakizee, lakini yeye alikuwa hataki badala yake anataka twende wote kwenye dansi,".

Lulu ameeleza kuwa wakati akiendelea kuongea na Kanumba, simu yake ikawa inaita ambapo aliogopa kupokea mbele ya Kanumba kwa sababu alihisi rafiki zake wanampigia, hivyo endapo wangemuuliza kuhusu suala la kutoka basi Kanumba angesikia.

Kutokana na hali hiyo, Lulu alisema kuwa aliamwambia Kanumba kwamba anataka akachukue Maji ya kunywa jikoni.

"Nikiwa naelekea kuchukia Maji nilipokea simu, ambapo nikaanza kuongea na rafiki zangu kwamba wasubiri nitatoka, lakini wakati nakata simu Kanumba alikuwa ananifatilia kwa nyuma na kuanza kuniuliza naongea na nani,

"Niliogopa kumwambia kwa sababu ningemwambia naongea na rafiki zangu kuhusu kutoka angenipiga, nikaanza kumtania kwa kumwambia unanifata hadi jikoni kujua naongea na nani,".

Akiendelea na ushahidi wake, Lulu  amesema kuwa Kanumba alikuwa akimuuliza anaongea na nani huku akimfata, na akiwa katika hali ya kukasirika ambapo yeye akawa anarudi nyuma.

"Wakati wote huo alikuwa katika hali ya kulewa, hivyo wakati ananifata nikahisi anataka kunipiga na mimi nikawa nazidi kurudi nyuma nikafungua mlango na nikatoka hadi nje,".

Amesema kuwa aliamua kutoka nje akiamini kwamba Kanumba asingeweza kumfata kwa sababu alivaa taulo na alikuwa tumbo wazi, hivyo angeona aibu na angeshindwa kumfata kulingana na umaarufu wake.

"Hata hivyo aliendelea kunifata, ambapo alinikimbiza hadi getini na akatoka hadi nje ya geti akiwa peku peku,".

Lulu amebainisha kuwa kutokana na hali hiyo aliamua kukimbia hadi lilipo gofu la baa ya Vatican ambayo ilikuwa haifanyi Kazi kwa wakati huo.

"Wakati tukio likiendelea umeme ulikatika, ambapo mimi niliingia hadi kwenye ghofu hilo na kujificha, lakini Kanumba alinifata hadi nilipojificha na kuanza kunipiga makofi ya uso,".

Amesema kuwa baada ya kumpiga alimshika mikono na kuanzia kumburuza kutoka nje hadi kumuingiza ndani, ambapo alimuingiza hadi chumbani kwake kisha kufunga mlango na funguo, kisha kumrusha kitandani.

"Baada ya kunitupa kitandani, aliinama chini na kuchukua Panga ambapo akaanza kunipiga nalo kwenye ubapa hasa maeneo ya mapajani, kutokana na mimi nilikuwa natapatapa ambapo nilijiziba uso ili asiweze kunikata huku nikipiga kelele za kuomba msaada,

"wakati akinipiga alikuwa akilalamika kwamba kwanini naongea na simu na mwanaume mwingine mbele yake,".

Lulu amebainisha kuwa wakati Kanumba akimpiga alikuwa katika hali ya jazba na kuema kwa haraka.

"Ghafla nikasikia sauti ya Panga limedondoka chini, pia nikasikia sauti kama ya mtu amekabwa, ambapo nilitoa mikono na kuona ameanguka kwa kujigonga kichwani kwenye ukuta, kisha akawa kama mtu anayetapatapa ambapo alirudi tena nyuma na kujigonga ukutani,,".

Lulu amesema kuwa kutokana na hali hiyo, aliinuka kutoka kitandani na kukimbilia chooni kwa ajili ya kujificha, huku  akiwa anapiga kelele za kuomba msaada.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...