Monday, October 13, 2014

LWAKATARE. DDP KUCHUANA UPYA LEO





Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare. PICHA|MAKTABA 


Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare leo anatarajiwa kuchuana upya na Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) wakati Mahakama ya Rufani itakaposikiliza maombi ya marejeo ya hukumu ya Mahakama Kuu iliyomfutia mashtaka ya ugaidi.

Maombi hayo Namba 5 ya mwaka 2014, yalifunguliwa na DPP akipinga uamuzi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam kumfutia Lwakatare mashtaka ya ugaidi yaliyokuwa yakimkabili yeye na mwenzake, Joseph Ludovick.

Katika maombi hayo, DPP anaiomba Mahakama ya Rufani iitishe majalada ya kesi hiyo na kuchunguza uhalali wa uamuzi wa Mahakama Kuu kuwafutia washtakiwa hao mashtaka ya ugaidi na kisha ifute uamuzi huo wa Mahakama Kuu na amri zote ilizozitoa.

Pamoja na mambo mengine, DPP anadai kuwa haikuwa sahihi Mahakama Kuu kuamua kuwa mashtaka hayo hayakuwa halali, kwani hapakuwa na taarifa zilizowasilishwa dhidi ya washtakiwa ambazo Mahakama Kuu ingezizingatia katika kuamua uhalali wake. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Maombi hayo yamepangwa kusikilizwa leo na jopo la majaji watatu linaoongozwa na Jaji Nathalia Kimaro, akishirikiana na William Mandia na Profesa Ibrahim Juma.

Lwakatare na Ludovick walikuwa wakikabiliwa na mashtaka manne katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, matatu kati yake yakiwa ya ugaidi na moja la kawaida la jinai.

Mashtaka hayo ya ugaidi yalikuwa ni kupanga kumteka aliyekuwa Mhariri Mtendaji wa gazeti la Mwananchi, Dennis Msacky na kisha kumdhuru kwa sumu, kushiriki mkutano wa vitendo vya ugaidi (kwa washtakiwa wote) na kuhamasisha vitendo vya ugaidi lililokuwa likimkabili Lwakatare pekee.

Shtaka jingine la jinai lilikuwa ni kula njama kutenda makosa, ambalo lilikuwa likiwakabili wote kwa pamoja.

Hata hivyo, Mei 8, mwaka huu Jaji Lawrence Kaduri wa Mahakama Kuu aliwafutia mashtaka ya ugaidi, baada ya mawakili wa Lwakatare kufungua maombi wakipinga uamuzi wa DPP wa kuwafutia mashtaka katika kesi ya awali na kuwakamata upya na kuwafungulia mashtaka hayohayo.

Katika uamuzi wake, Jaji Kaduri alikubaliana na hoja za mawakili wa Lwakatare kuwa mashtaka hayo hayana maelezo ya kutosha kuonyesha kuwa ni ya ugaidi.

Jaji Kaduri alisema kuwa mashtaka hayo yalipaswa yawe na maelezo yanayoonyesha uhalisia wa ugaidi na kwamba katika mashtaka hayo kuna makosa kwa kuwa hapakuwa na maelezo ya wazi ya asili ya ugaidi.

Hata hivyo, Jaji Kaduri alikubaliana na hoja za Wakili wa Serikali, Prudence Rweyongeza kuwa uamuzi wa DPP kufuta kesi ya kwanza na kuwakamata washtakiwa na kuwafungulia tena kesi yenye mashtaka hayohayo ulikuwa sahihi.
Lwakatare na Ludovick walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Machi 18, 2013 na kusomewa mashtaka hayo katika kesi namba 37 ya mwaka 2013.
Hata hivyo, Machi 20, DPP aliwafutia mashtaka hayo, kutokana na makosa yaliyofanywa na Mahakama ya Kisutu kuwataka washtakiwa wajibu mashtaka hayo ambayo yanasikilizwa na Mahakama Kuu, lakini muda mfupi baadaye walikamatwa na kufunguliwa tena mashtaka hayo. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz
Na Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...