Tuesday, October 29, 2013

WAZIRI AANGUA KILIO MAHAKAMANI



ALIYEKUWA Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Arcado Ntagazwa, jana alijikuta akiangua kilio ndani ya kizimba, baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutamka yeye na wenzake wawili wameachiwa huru.
Ntagazwa alitokwa na machozi, mbele ya Hakimu Mkazi, Geni Dudu, alipokuwa akisoma hukumu katika kesi ya kujipatia tisheti 5,000 na kofia 5,000 za kumbukumbu ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, mwaka 2009 kwa njia ya udanganyifu.

“Ukiangalia ushahidi hapakuwa na udanganyifu katika kuagiza kuchapwa kwa tisheti na kofia, waliamini wangeweza kulipa fedha hizi, ukiangalia uhalisia wa tisheti hazikuwa za kibishara… zilikuwa za kugawa bure kwa wananchi, zilikuwa kwa ajili ya kufikisha ujumbe wa kupiga vita rushwa na ufisadi, zilikuwa kama mabango.

“Ni kweli washtakiwa walihujumiwa na kushindwa kulipia gharama za uchapishaji, tayari nina shaka hiyo inatosha sana kuwaona washtakiwa si wakosaji, shaka hata ikiwa ndogo kiasi gani manufaa yanakuwa kwa washtakiwa.

“Kutokana na ushahidi na vielelezo vilivyopo mahakamani, naona washtakiwa hawana kosa, wako huru, mlalamikaji akafungie kesi ya madai ili aweze kupata haki yake,” alisema Hakimu Dudu na kutamka washtakiwa wako huru.

Ntagazwa, alianza kujifuta machozi yaliyokuwa yakibubujika akiwa kizimbani na hata baada ya kushuka kizimbani aliendelea kububujikwa na machozi, huku akitembea taratibu mno kuelekea nje ya jengo la mahakama.

Hakimu Dudu kabla hajafikia uamuzi wa kuwaachia huru washtakiwa, alisema katika ushahidi hapakuwa na ubishi washtakiwa walichapisha tisheti na kofia, ushahidi huo unasapotiwa na vielelezo kwamba kampuni mbili zilikubaliana kuingia mkataba huo.

Alisema upande wa Jamhuri ulileta mashahidi watano mahakamani kuthibitisha mashtaka hayo na kuomba katika majumuisho ya mwisho, kwamba washtakiwa watiwe hatiani kwani waliweza kuthibitisha makosa yao bila kuacha shaka.



“Kwa maoni yangu, naona hapakuwa na udanganyifu, makubaliano ya kuchapisha tisheti na kofia yalifikiwa katika kikao cha bodi ya wadhamini na yangeweza kulipwa, washtakiwa katika utetezi wao waliweza kutoboa matundu ushahidi wa upande wa mashtaka na ushahidi wa nyaraka ni mzito kuliko wa maneno,” alisema Dudu.

Akizungumza nje ya mahakama, Ntagazwa alishukuru kwa kutendewa haki, alisikitishwa na kitendo cha Polisi cha kumkamata akiwa bafuni hana nguo kwa kosa la madai.

“Ukitumia haki yako ya kikatiba CCM watakuzushia lolote, kwa hali hii hatutafika, nawashauri Watanzania wasome Zaburi 7, 9, 10, 11, 12 na Zaburi 10 someni yote, wenye nia mbaya wasipate nafasi ya kudhulumu wenzao, mzigo wako mwachie Mungu hata kuacha ushindie,” hayo ni maneno ya Ntagazwa, akinukuu Zaburi.

Kesi hiyo kwa upande wa mashtaka iliongozwa na Wakili wa Serikali, Charles Anindo, na upande wa utetezi uliongozwa na Wakili Alex Mushumbusi, aliyekuwa akimtetea Ntagazwa na mwanawe, Dk. Webhale Ntagazwa na mshitakiwa wa kwanza, Senetor Mirelya (60).

Aprili 23, 2012, ilidaiwa mahakamani hapo kuwa Oktoba 22, 2009 huko Msasani Mikoroshini, washtakiwa hao kwa nia ovu walijipatia fulana 5,000 na kofia 5,000 zenye thamani ya Sh milioni 74.9 kutoka kwa Noel Severe kwa makubaliano kuwa wangemlipa kiasi hicho cha fedha katika kipindi cha mwezi mmoja tangu walipochukua vifaa hivyo, lakini hata hivyo walishindwa.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...