Monday, May 20, 2013

MAWAZIRI WATATU WA JK KUNG'OLEWA.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi  Dk Shukuru Kawambwa.
 Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Dk. Mathayo David Mathayo 
Dk. Mathayo David Mathayo, Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi.https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjFUbOhVVOJm2f6bdqpXvu56CscHBIeGzm4K-xRWmBDHm6ydKFrQ776hSwU2kVohVht2rPOL3pxvEcg1JcJ4GiUaUfdpTgRk4_xRxonDr-2eFGrBNoBPZ8DOI2hkZ-ctvPdadyvd-RSiXg/s1600/Dk.+Fenella+Mukangara,+Waziri+wa+Habari,+Vijana,+Utamaduni+na+Michezo.JPG 
Dk. Fenella Mukangara, Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo

UPEPO mbaya ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) unazidi kuvuma, safari hii wabunge wake wakimtaka Rais Jakaya Kikwete kuwafukuza kazi mawaziri watatu.

Mawaziri wanaotakiwa kung’olewa ni Dk. Shukuru Kawambwa (Elimu na Mafunzo ya Ufundi), Dk. Mathayo David Mathayo (Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi) na Dk. Fenella Mukangara (Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo).
Kama Rais Kikwete atakubali kuwaondoa madarakani mawaziri hao, hii itakuwa mara ya pili kwake kufanya hivyo. Mara ya kwanza ilikuwa Mei mwaka jana.

Mwaka jana Rais Kikwete aliamua kuwaengua madarakani baadhi ya mawaziri waliokuwa wakiandamwa kwa tuhuma mbalimbali, ikiwemo uwajibikaji mbovu.

Miongoni mwa walioenguliwa mwaka jana ni Dk. Haji Mponda aliyekuwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Mustafa Mkulo (Waziri wa Fedha), William Ngel
eja (Nishati na Madini na Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii).
Msimamo huo wa wabunge wameutoa jana katika kikao baina yao na Rais Kikwete kilichokuwa kikitathimini mwenendo wa chama na utendaji wa wabunge.


Chanzo chetu ndani ya kikao hicho kilieleza kuwa baada ya Rais Kikwete kutoa hotuba ya ufunguzi, baadhi ya wabunge walianza kuchangia, huku wengine wakishutumiana kwa kuvujisha siri za vikao nje kwa waandishi wa habari.



Wabunge hao walidai kuwa mawaziri hao watatu wamekuwa mzigo kwa Serikali ya CCM kutokana na utendaji wao kutokuwa wa kuridhisha.


Walisema matunda ya uwepo wa mawaziri hao kwenye wizara husika hayaonekeni, hivyo kumtaka Rais Kikwete awang’oe.


Waziri Kawambwa analaumiwa kwa kuzembea kwenye sekta ya elimu ambayo inazidi kushuka kiasi cha kuifanya serikali ifute matokeo ya kidato cha nne ya mwaka jana.


Walisema kufutwa kwa matokeo hayo ambayo asilimia 60 ya waliofanya mtihani walipata daraja sifuri, kunadhihirisha uwezo mdogo wa Dk. Kawambwa.


Wakati Kawambwa akibanwa kwa hilo, wenzake Mathayo na Mukangara wanadaiwa kuwepo wizarani bila kuonesha ufanisi wowote.Wabunge hao walidai kuwa Wizara ya Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi anayoiongoza Dk. Mathayo ni nyeti na ilipaswa kuwa ya pili katika kuchangia pato la taifa baada ya Wizara ya Maliasili na Utalii.



Walimshambulia Dk. Mathayo kuwa mzigo kwa wizara hiyo kwani alipokuwepo Dk. Magufuli (Waziri wa Ujenzi) ilikuwa ikifanya vizuri tofauti na hivi sasa.



“Tusioneane aibu, huyu Mathayo ameshindwa kazi, mwenyekiti muondoe kabla mambo hayajazidi kuwa mabaya,” alisema mbunge mmoja.


JK abariki mchakato wa urais 

Mapema katika hotuba yake ya ufunguzi wa kikao hicho, Rais Kikwete aliruhusu makundi ya wana-CCM wanaotaka kuwania urais 2015 kuendelea na mchakato wa kuweka mikakati yao ya kampeni bila chuki.

Kwa mujibu wa chanzo chetu katika kikao hicho ambacho waandishi hawakuruhusiwa kuingia, lengo kubwa lilikuwa ni kujadili masuala mbalimbali ya kitaifa ikiwemo utekelezaji wa ilani ya uchaguzi katika majimbo ya uchaguzi ikiwa ni pamoja na ahadi za rais.


Rais Kikwete aliwataka wana-CCM wenye nia ya kugombea urais kuendelea na mikakati yao kwa ustaarabu na kuepusha uadui kutokana na wapambe wao kuwa na kambi zaidi ya moja.



“Tuangalie makundi ya urais 2015 yasishambuliane kwa kuvunja chama, wenye nia hiyo ya kugombea waendelee na mikakati yao na si kujenga chuki kwa makundi mengine.


“Mkumbuke kuwa kambi hizo za urais zinatakiwa kujitizama na wafuasi wao maana wafuasi wengi si wa kuaminika,” alisema Kikwete.



Rais Kikwete aliwafananisha baadhi ya wapambe na matango pori yanayoota popote, ambapo alisema wamekuwa na tabia ya kutoa maneno huku na kupeleka upande wa pili.



Tanzania Daima ilidokezwa kuwa Kikwete alikuwa na ajenda nne ambazo ni urais 2015, kuwahimiza wabunge kutembelea majimbo yao ya uchaguzi, kurudi majimboni kwao kusimamia ahadi zao, chama na zile za viongozi wa kitaifa akiwemo yeye na kuisimamia serikali na kuikosoa bila kuibomoa.


Kwamba Kikwete aliwataka wabunge hao kutumia kauli za staha wanapoikosoa serikali kama ambavyo baadhi wamekuwa wakifanya.



“Mnatakiwa kuisimamia serikali na kuikosoa bila kuibomoa, lakini kuna baadhi yenu mmekuwa mnaibomoa serikali kwa jinsi mnavyochangia huko bungeni, hilo si jambo jema hata kidogo, waachieni wale wenzenu,” alisema.



Katika hilo, wabunge walionya tabia ya baadhi ya mawaziri wanavyohusiana na wabunge na wanavyoonekana kwa wananchi, lakini wakaitaka serikali kutimiza wajibu wake ipasavyo kwa kutoa fedha za bajeti kama zinavyopitishwa na Bunge.


Pia ubadhirifu unaofanywa kwenye halmashauri nchini, utendaji mbovu wa baadhi ya wakuu wa wilaya na mikoa nchini, hivyo wakamtaka rais kukunjua makucha yake kuondokana na uozo huo.

Kuhusu kutembelea majimbo, rais alisema kuwa baadhi ya wabunge wameyatelekeza kwa kutorudi kusikiliza kero za wananchi na kutimiza ahadi zao.

Aliwaonya kuwa kwa tabia hiyo wala wasije kuwaonea donge wale wanachama wengine watakaochaguliwa kuwa wabunge badala yao.


Lugola, Filikunjombe, Mpina wakaangwa

Baada ya mapumziko ya mchana, kikao hicho kiliendelea kwa wabunge kutoa madukuduku yao ambapo chanzo chetu kinasema kuwa wabunge watatu walishambuliwa kwa tabia yao ya kuikosoa serikali kwa kauli nzito.

Wabunge hao ni Kangi Lugola (Mwibara), Deo Filikunjombe (Ludewa) na Luhaga Mpina wa Kisesa ambao hata hivyo wote hawakuhudhuria kikao hicho.



Lugola amekuwa mwiba mkali wa kuwashambulia mawaziri wa serikali kutokana na utendaji wao kutoridhisha ambapo hivi karibuni wakati akichangia hotuba ya bajeti ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), alitishia kuwataja mawaziri na watendaji wanojihusisha na rushwa pamoja na biashara ya dawa za kulevya.


Filikunjombe naye amekuwa akipinga kuunga mkono hoja za serikali huku akitumia maneno makali kama vile ‘serikali kuvaa miwani ya mbao’, kutokuwa sikivu na mengine kama hayo ambayo inaelezwa kuwa hata Rais Kikwete jana aliyatolea mfano.


Chanzo chetu kilieleza kuwa aliyeibua sakata hilo ni mbunge mmoja wa Tabora, akidai wenzao hao wamekuwa na tabia isiyokoma, na hivyo kupendekeza kuwa kama wanataka ni heri wakahamia upinzani kuliko kuendelea kuivua nguo Serikali ya CCM.


Hadi tunakwenda mitamboni jana, kikao hicho kilikuwa kikiendelea na kwa mujibu wa ofisa mmoja wa chama, walitarajia kuwa kingemalizika usiku wa manane.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...