Friday, June 06, 2014

TIGO, AIRTEL NA ZANTEL ZAUNGANISHA HUDUMA




Meneja Mkuu wa Kampuni ya Tigo, Diego Gutierrez (Kulia) na Ofisa Mtendaji Mkuu wa DTBi, Mhandisi George Muhula wakitia saini ya makubaliano jijini Dar es Salaam jana baina ya Tigo na DTBi ya kusaidia wajasiriamali kujifunza teknolojia ya digitali na mawasiliano. Wanaoshuhudia ni Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Prof Makame Mbarawa na Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dk Hassan Mshinda. Picha na Venance Nestory.


Kampuni za simu za mkononi za Tigo, Airtel na Zantel zimeunganisha huduma zao za kutoa, kutuma na kuweka fedha na sasa mteja anaweza kutuma fedha kutoka mtandao mmoja kupitia mwingine.

Taarifa ya pamoja na kampuni hizo iliyotolewa jana, ilisema kuwa wote wanaotumia huduma za kifedha za mitandao hiyo, wataweza kutumiana fedha kupitia simu zao za mikononi pasi na tatizo baada ya kampuni hizo kuunganisha huduma zao.

Huduma hiyo inayotarajiwa kuanza kutumika mwishoni mwa mwezi huu, itawafanya wateja wa mitandao hiyo kutumiana na kupokea fedha moja kwa moja kwenye akaunti zao tofauti na ilivyokuwa awali. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Taarifa hiyo ilisema ushirikiano huo unaweka rekodi ya hatua muhimu katika ukuaji wa sekta ya mawasiliano nchini na Afrika kwa kuwa si rahisi kwa kampuni zinazoshindana kufanya uamuzi wa kibiashara wa aina hiyo.

“Ikumbukwe kuwa makubaliano ya namna hii hapo awali yalifanywa na kampuni za simu kuwawezesha wateja wao kupata huduma za kupigiana simu na kutumiana ujumbe mfupi pekee,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo ya pamoja na kuongeza kuwa, wateja wao watapata pia punguzo la gharama za uhamishaji fedha, pia hawatahitajika kuwa na namba ya siri.

Kwa sasa, ili mteja aweze kupokea fedha alizotumiwa kutoka mtandao mwingine, anahitajika kuonyesha namba ya siri (pin) wakati wa kutoa fedha jambo ambalo limekuwa likitatiza ufanisi wa miamala hiyo.

Mkurugenzi Mkuu wa Zantel, Pratap Ghose alisema kampuni hizo zina dhamira ya dhati kuhakikisha huduma na ushirikiano huo vinawawezesha wateja kufanya biashara zao kwa ufanisi na urahisi zaidi nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa Tigo, Diego Gutierrez alisema anafurahi kushirikiana na washindani wake, Airtel na Zantel katika jitihada za kuendeleza huduma za kutuma na kupokea fedha kupitia simu za mkononi nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa Airtel, Sunil Colaso alisema kampuni yake imejikita katika kuwapa wateja wake huduma zenye ubunifu wa hali ya juu bila kujali ushindani wa kibiashara.

Matumizi ya simu za mkononi kufanya miamala ya kifedha yamezidi kukua kwa kasi nchini na kwa mujibu wa Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa hadi sasa kuna watumiaji wa huduma za fedha kwa simu za mkononi 12,330,962. Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Na, Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...