Tuesday, February 25, 2014

MILIPUKO YA MABOMU YARINDIMA Z'BAR

bomu_b1855.png
Na Mwinyi Sadallah, Mwananchi
Zanzibar. Watu wanne wamejeruhiwa baada ya milipuko minne inayoaminika kuwa ni mabomu kutokea katika maeneo matatu tofauti Zanzibar.
Katika moja ya matukio hayo, watu wanne walijeruhiwa, mmoja akikatika mguu, katika eneo la Unguja Ukuu, Mkoa wa Kaskazini Unguja. Majeruhi wawili wamelazwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja, Unguja.
Mkuu wa Operesheni wa Polisi, Mkoa wa Kusini Unguja, Hamad Said Masoud alisema mlipuko wa kwanza ulitokea juzi katika eneo la Fuaoni Maili Nne wakati watu wasiojulikana waliporusha kitu kinachoaminika kuwa ni bomu wakati waumini wa Kanisa la Evangelist wakiendelea na ibada ya Jumapili.
Kamishna wa Polisi Zanzibar, Hamdan Omar Makame alisema tukio la juzi, kitu kinachosadikiwa kuwa ni bomu kilirushwa wakati waumini wa kanisa hilo wakiendelea na ibada na kutoa mlipuko na kishindo kikubwa. Alisema wakati wakiendelea na uchunguzi wa tukio hilo, milipuko mingine mitatu ilitokea jana.
Katika mlipuko wa kwanza kwa jana uliotokea saa 6.30 mchana katika kituo kimoja cha fundi vyuma aliyetambulika kwa jina la Juma Abdallah huko Unguja Ukuu ndiko kulikokuwa na watu waliojeruhiwa.
Waliojeruhiwa katika tukio hilo ni Pandu Haji Pandu aliyekatika mguu na Shaaban Khamis Ibrahim ambaye aliumia sehemu za kiuno.
Hamad alisema mtu mmoja aliokota chuma kizito na kukipeleka kwa fundi akitaka atengenezewe nanga kwa ajili ya uvuvi.
Alisema mhunzi huyo alipokea kazi hiyo na alipokuwa akijiandaa kwa matengenezo ndipo mlipuko huo ulipotokea. Mlipuko huo ulitokea sambamba na mwingine katika Mgahawa wa Mercury's uliopo Malindi, Mkoa wa Mjini Magharibi na kusababisha huduma za chakula kusitishwa kwa muda.
Tukio la mwisho lilikuwa saa 7:15 mchana katika Kanisa la Anglikana, Mkunazini. Katibu wa Kanisa hilo Dayosisi ya Zanzibar, Nuhu Saranya alisema: "Nilisikia kishindo cha mlipuko, wakati nikitafakari ni kitu gani hicho, nikasikia mlipuko wa pili nje ya kanisa letu," alisema.
Mmoja wa majeruhi, Mohamed Ibrahim alisema hakujua kilichotokea huku akilalamika kuwa masikio yake hayasikii vizuri kutokana na kishindo hicho.
Kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-like page ya facebook ya Jambo Tz

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...