Wednesday, October 02, 2013

BAADA YA KUYAFUNGIA MAGAZETI YA MWANANCHI NAMTANZANIA, SERIKALI SASA YAINYOOSHEA KIDOLE GAZETI LA RAI.

SERIKALI imeitaka kampuni ya New Habari 2006, kuacha kuchapisha gazeti la Rai kila siku na kampuni ya Mwananchi kuacha kuchapisha gazeti la Mwananchi kwenye mtandao.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari Malelezo, Assah Mwamebene, alitoa onyo hilo ofisini kwake jana na kuongeza kuwa ameziandikia barua kampuni hizo, zijieleze ni kwanini zinafanya hivyo.
Tumeona gazeti la Mwananchi baada ya kufungiwa, limeendelea kuchapishwa kwenye mtandano wa intaneti kinyume na amri iliyotolewa. Vivyo hivyo kwa Rai ambayo ilikuwa ikichapishwa mara moja kwa wiki, imeanza kutoka kila siku, tunawataka warejee ratiba yao,” alisema.
Alisema endapo vyombo hivyo havitatekeleza agizo hilo na kujieleza katika ofisi yao ifikapo kesho, Serikali italazimika kuchukua hatua kali zaidi ikiwa ni pamoja na kuongeza adhabu, ikiwemo kufungia kwa muda usiojulikana na kufutiwa usajili wake.
“Umma ufahamu kuwa Serikali haikukurupuka kufungia magazeti hayo, uamuzi ulifanywa baada ya kufuata taratibu zote za msingi ikiwemo kuwasikiliza wahusika.
“Katika suala hili hatutarudi nyuma, hata waje wanaharakati wa aina gani, lengo la Serikali ni kuhakikisha maadili yanazingatiwa katika taaluma na hatutakuwa na mchezo katika maslahi ya nchi,” alisema.
Gazeti la Mwananchi limefungiwa kwa muda wa wiki mbili na Mtanzania, linalomilikiwa kampuni ya New Habari 2006, limefungiwa kwa miezi mitatu kuanzia Septemba 27 mwaka huu kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti ya 1976 na kanuni zake za mwaka 1977. 
Alipoulizwa Mhariri Mtendaji Mkuu wa New Habari 2006 Ltd, Absalom Kibada, alidai wamefuata utaratibu kuchapa gazeti la Rai kila siku, lililoanza kutoka baada ya kufungiwa gazeti la Mtanzania, lililokuwa likitoka kila siku.
Alidai kuwa kampuni ya New Habari 2006 Ltd, ina kibali kilichotolewa mwaka 1994, hivyo alichofanya ni kumuarifu Msajili mabadiliko ya ratiba ya utokaji wa gazeti hilo.
Kampuni yetu imerithi mambo yote ya wamiliki wa awali, mwaka 1994 msajili aliruhusu Rai kutoka kila siku, na Jumatatu tulimuarifu Msajili kuhusu kuanza ratiba hiyo, hivyo tumefuata utaratibu wote.
Hatua hii ya sasa ni kutaka kuiadhibu Rai kwa makosa ya Mtanzania,” alidai. Mhariri Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), Bakari Machumu hakupatikana kuzungumzia suala hilo baada ya simu yake ya kiganjani kuita bila majibu.

SOURCE: HABARI LEO

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...