Wednesday, June 19, 2013

HOFU YATANDA MKOANI SHINYANGA JUU YA MAUAJI YA WATOTO

( Picha na maktaba )

Na Steve Kanyeph
Wakazi wa manispaa ya Shinyanga wamegubikwa na hali ya hofu na wasiwasi kufuatia matukio ya mara kwa mara ya kuuawa kwa watoto wa kike wanaofanyiwa ukatili na unyanyasaji na kisha kuuawa ama kutelekezwa wakiwa hawajitambui.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakazi hao walisema vitendo vya unyanyasaji kwa watoto wa kike wenye umri wa kuanzia miaka tisa hadi kumi na nne katika manispaa ya Shinyanga kwa zaidi za miezi minne sasa vimekithiri hali ambayo inatishia amani kwa wakazi hao.

Akizungumza na Jambo Tz jana mkazi wa eneo la Ngokolo katika Manispaa ya Shinyanga bi Dafrossa Pius ambaye ni mjasiliamali, siku moja baada za tukio la kuuawa kikatili kwa binti mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka kumi na mbili hadi kumi na tatu, kisha mwili wake kufungwa kama mzigo kwenye boksi na kutupwa kwenye ghuba la takataka katika eneo hilo la ngokolo mitumbani,alisema ni ukatili usiovumilika hata kidogo “ukatili kama huu kwa watoto wa kike wasio na hatia haupaswi kuvumiliwa wala kufumbiwa macho``

Bi Dafrossa alisema mara kwa mara watoto wa kike katika Manispaa za shinyanga wamekuwa wakibakwa,na kisha kutelekezwa,hali ambayo inasababisha wananchi kuishi maisha yenye hofu na wasiwasi,huku wakifanya kazi na shughuli zao bila amani wakihofia usalama wa watoto:

Timu ya ulinzi na usalama wa mtoto katika Manispaa za Shinyanga imelaani vikali tukio la kuuawa kwa binti huyo na kusema kuwa itaendelea na harakati zake kuhakikisha kwamba suala la ulinzi na usalama wa mtoto linafanikiwa.

Timu ya ulinzi na usalama wa mtoto katika manispaa za shinyanga inaundwa na
Idara za serikali ikiwemo idara ya Elimu,Afya,mipango,maendeleo ya jamii,ustawi wa jamii.Polisi pamoja na asasizinazofanya kazi katika ulinzi wa mtoto.

June 17, majira ya saa tano asubuhi mwili wa mtoto wa kike ulikutwa umefungwa kwenye boksi na kisha kutupwa kwenye ghuba la takataka katika eneo ngokolo mitumbani mjini shinyanga

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa shinyanga kamishina msaidizi wa polisi Evarist Mangalla alithibitihsa kutokea kwa tukio hilo.

Kamanda Mangalla alisema binti huyo aliyeuwawa kikatili anasadikiwa kuwa na umri wa miaka kati ya kumi na mbili na kumi na tatu ambaye hata hivyo hakufahamika mara moja jina wala makazi yake na kwamba aliuawa kwa kupigwa na kitu kizito kichwani na kisogoni.

Aidha kamanda mangalla alibainisha kuwa taarifa za uchunguzi wa daktari zinaeleza kuwa marehemu alibakwa kabla ya kuuawa kwake.

Mwili wa marehemu huyo haujatambuliwa na umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya mkoa wa Shinyanga.

Jeshi la polisi limetoa wito kwa wanananchi mkoani shinyanga kutoa ushirikiano wa dhati utakaofanikisha kukamatwa kwa watuhumiwa wa tukio hilo na matukio mengine ya aina hiyo na kwamba jeshi hilo linaendelea na uchunguzi juu ya tukio hilo ili kuwabaini waliofanya mauaji hayo.

Kwa zaidi ya miezi minne sasa kumekuwa na matukio ya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia wanayofanyiwa watoto wenye umri wa kuanzia miaka tisa hadi kumi na nne ktk manispaa za shinyanga.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...