Sunday, June 23, 2013

ASKOFU AITAKA SERIKALI KUWABANA WASIOTAKA NCHI ITAWALIKE.

RAIS Jakaya Kiwete akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa serikali na dini wakati alipohudhuria sherehe za miaka 25 ya Askofu wa jimbo kuu la Morogoro Telesphol Mkude wa pili kulia kwa rais katika viwanja vya shule ya ST Peter mkoani Morogoro jana.


SIKU chache baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutaka Serikali iachwe ifanye kazi yake katika kudhibiti vurugu zinazoibuka kila kukicha, Askofu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Morogoro, Mhashamu Telesphor Mkude naye ameitaka Serikali kuwadhibiti wote wasiotaka nchi itawalike.Askofu huyo amesema kuonya pekee hakusaidii, bali inawajibu wa kuwachukulia hatua kali ili kukomesha vitendo vinavyotishia amani nchini.Askofu Mkude aliyasema hayo jana wakati wa maadhimisho ya Jubilei ya miaka 25 ya uaskofu wake kwenye viwanja vya Seminari ya Mtakatifu Petro mjini hapa ambapo Rais Jakaya Kikwete alikuwa miongoni mwa wageni mashuhuri waliohudhuria.

Katika maadhimisho hayo, maaskofu zaidi ya 35 wakiwemo wa Majimbo Makuu wa ndani na nje ya nchi walihudhuria.

Aidha walikuwapo mapadri, watawa, waamini na mamia ya wananchi wa mikoa ya jirani, sambamba na viongozi wa Serikali na vyama vya siasa wakiwemo wa chama tawala, CCM.

Pamoja na ushauri wake, Askofu Mkude pia alimshukuru Rais kuweza kushiriki katika maadhimisho hayo, huku alirudia kumwomba yeye pamoja na Serikali yake kusimamia suala zima la amani ya Tanzania.

Askofu Mkude alisema Serikali inao wajibu kuhakikisha amani inaendelea kudumishwa wakati wote na kuchukua hatua za haraka za kukutana na viongozi wa dini pale panapotokea kutoelewana katika imani zao ili kufikia mwafaka utakaodumisha amani ya Tanzania.

“Suala hili la kuchinja ...linaweza kupatiwa ufumbuzi wa kudumu kwa viongozi wa dini na Serikali kukutana na kuliweka sawa...mbona hatugombani kwenye kuzika, makaburi ...hili la kuchinja kwanini linakuzwa zaidi wakati huu , ambako huku nyuma halikuweza kuwepo ...” alihoji Askofu Mkude mbele ya Rais.

Naye Rais Kikwete, akizungumza, aliwataka viongozi wa madhehebu ya dini nchini kuendelea kuhubiri amani, upendo, utulivu na mshikamano ili kujenga misingi imara ya maelewano yaliyodumu kwa miaka mingi miongoni mwa Watanzania.

Pamoja na kuomba viongozi wa dini kuhubiri amani, Rais Kikwete alisema Serikali itaendelea kushirikiana na Madhehebu ya dini katika kuleta maendeleo ya wananchi ili kuinua hali zao za kimaisha.

Mbali na hayo Rais Kikwete pia alisema viongozi wa madhehebu ya dini wanayo nafasi kubwa na ya kipekee ya kuwafundisha vijana kuwa Wacha-Mungu na raia wema wa nchi yao.

Katika hotuba yake pia alimpongeza Askofu Mkude kwa kutimiza miaka 25 ya uaskofu na kusema yeye pia ni miongoni mwa wakazi wa Parokia ya Lugoba, Wilaya ya Bagamoyo ambayo ni sehemu ya Jimbo la Kanisa Katoliki la Morogoro.

Rais pia alisema Kanisa Katoliki Jimbo la Morogoro limetoa fursa kwa maelfu ya vijana kupata elimu kwa manufaa yao sambamba na kuanzisha vituo vya afya ikiwa ni juhudi za kuunga mkono mpango wa Serikali za kupunguza vifo vya watoto na akinamama wajawazito.

Kwa upande wake, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, aliwataka viongozi wa Kanisa hilo, wanapobanwa na hali ngumu ya kutukanwa na watu wengine, jukumu lao ni kumkimbilia Yesu Kristo huku wakiendelea kuhubiri upendo na amani.

“Sisi Viongozi wa Kanisa letu akiwemo Askofu Mkude tunapokumbana na hali ya ugumu wa kutukanwa na watu wengine ni vyema kuwa karibu na Yesu ili tuache mahangaiko na badala yake tuhubiri amani na upendo miongoni mwa waamini na jamii nzima,“ alisema Mwadhama Kardinali Pengo.

Hata hivyo alimtaka Askofu Mkude kutumia nafasi ya Jubilei hiyo si tu kumshukuru Mungu kwa kutekeleza mema pia kumwomba radhi Mungu kwa yale ambayo hakuweza kuyatekeleza na kuwataka waamini wa Jimbo hilo kuendelea kumpatia ushirikiano katika majukumu yake.

Naye Rais wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa Katoliki Tanzania (TEC), Askofu, Tarcisius Ngalalekumtwa ambaye ni Askofu wa Jimbo la Iringa na Msimamizi wa Kitume wa Jimbo la Songea, alisema upendo ndiyo jambo kuu katika kusukuma gurudumu la kuwatumikia wananchi na waumini wa Kanisa hilo.

Hivyo aliwataka Maaskofu na waamini wengine pamoja na wananchi kuendelea kumwombea Askofu Mkude aweze kutimiza majukumu yale pamoja na Taifa kwa ujumla.

Wakati huo huo Kanisa Katoliki Jimbo la Morogoro, limetoa zawadi ya fedha Sh milioni 25 pamoja na kununua matairi matano na kumkabidhi Askofu Mkude kwa kutimiza miaka 25 ya uaskofu.
Makamu wa Askofu wa Jimbo hilo, Padre Patrick Kung’alo, alibainisha hayo wakati akisoma risala ya Jimbo hilo mbele ya wageni waalikwa akiwemo Rais Jakaya Kikwete.

Kwa mujibu wa Makamu huyo wa Askofu pia Umoja wa Mapadri wakati wa maadhimisho hayo ya Jubilee umezindua usajili wa Bima ya Afya ambapo katika hatua ya awali umetoa kiasi cha Sh 7,890,000 kwa ajili ya kuwalipia mapadre 23 kwa kadi ya kijani.

Akizungumzia mafanikio mengine ya kimaendeleo chini ya Askofu Mkude ndani ya kipindi cha miaka 25 kati ya hiyo 20 akitumika Jimbo la Morogoro na mitano Jimbo la Tanga, alisema amewezesha kujengwa kwa sekondari 11 za Kanisa , Shule za Msingi 12, shule sita za ufundi pamoja na shule 25 za awali.

Makamu wa Askofu huyo alitaja mafanikio mengine katika kipindi hicho ni kusomesha mapadri wapya 54, uanzishwaji wa Kituo cha Redio Ukweli, mashirika 27 ya kuhudumia watawa wa Kanisa hilo wa Jimbo la Morogoro.

Padri Kung’alo, alitaja mafanikio mengine ni upandishwaji wa hadhi ya Kituo cha Afya cha Mikumi cha Kanisa hilo kuwa Hospitali kamili, ujenzi wa vituo vitano vya afya, zahanati 10 na kuwezesha kupandishwa hadhi Hospitali ya Bwagala kuwa Hospitali Teule ya Rufaa.

Hata hivyo alisema, Askofu Mkude aliwezesha kuanzishwa kwa kituo cha kuwatunza watoto wenye ulemavu wa viungo na mtindio wa ubongo ili kuwezesha kundi hilo kupata huduma muhimu za kijamii ambazo wanakuwa hawazipati kama elimu na afya.
CHANZO HABARILEO.

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...