
Ndugu Wananchi;
Naomba
nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na kunipa
fursa ya kuzungumza nanyi kwa kupitia utaratibu wetu huu mzuri wa kila
mwisho wa mwezi. Leo ninayo mambo matatu ninayopenda kuzungumza nanyi.
Ziara ya Rais wa China Nchini Tanzania
Ndugu wananchi;
Jambo
la kwanza ni ziara ya Mheshimiwa Xi Jinping, Rais wa Jamhuri ya Watu wa
China aliyoifanya nchini kwetu kati ya tarehe 24 na 25 Machi, 2013.
Lengo la ziara yake ilikuwa kuimarisha uhusiano wa kihistoria uliopo
kati ya China na Tanzania. Napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru
wakazi wa Dar es Salaam kwa kumpokea vizuri mgeni wetu na ujumbe wake.
Wameondoka wakiwa na kumbukumbu nzuri ya nchi yetu na watu wake.



