Monday, November 10, 2014

'KURA YA MAONI MWANZO WA KUDAI KATIBA MPYA'


Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo - Bisimba akizungumza na waandishi wa Gazeti la Mwananchi katika mahojiano maalumu yaliyofanyika hivi karibuni Dar es Salaam.

Wakati Serikali ikihaha kuhakikisha inaandika historia mpya kwa kupitisha Katiba Inayopendekezwa Aprili 30, mwakani, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo – Bisimba amesema siku hiyo itakuwa mwanzo wa Watanzania kudai Katiba Mpya.

Dk Kijo – Bisimba, mmoja wa wanaharakati maarufu wa haki za binadamu nchini, amesema katika mazingira ambayo mchakato wa Katiba una dosari nyingi, ilikuwa ni busara kuusimamisha kwanza ili kujitathmini kabla ya kuendelea na Kura ya Maoni.

Mhitimu huyo wa shahada ya uzamivu ya sheria kutoka Chuo Kikuu cha Warwick, Uingereza, alisema hayo katika mahojiano maalumu na gazeti hili yaliyofanyika wiki iliyopita.

“Katiba hata ikiwa nzuri kiasi gani, kama haitokani na wananchi, haiwezi kukubalika,” alisema Dk Kijo – Bisimba akisisitiza hoja yake. Asante kwa kutembelea blog hii na endelea kuwa nasi siku zote, kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Tayari Rais Jakaya Kikwete ameshatangaza kuwa Kura ya Maoni itafanyika Aprili 30 mwakani baada ya Bunge la Katiba kukamilisha kazi ya kuiandika Oktoba 4, mwaka huu.

Hata hivyo, mchakato huo uliingia dosari baada ya kundi la wajumbe kutoka vyama vya upinzani na baadhi ya wateule, kususia vikao vya Bunge la Katiba kwa madai kuwa chombo hicho cha kihistoria kilipoteza mwelekeo kwa kuacha kujadili Rasimu ya Katiba iliyowasilisha na iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kuingiza mambo ya CCM.

Mchakato huo uliingia matatani zaidi katika kutafuta theluthi mbili ili kupitishwa baada ya kuibuka utata wa kura za wajumbe wa Zanzibar.

Ingawa ilipita, kumekuwa na maswali mengi kuhusu uhalali wa baadhi ya kura za baadhi ya wajumbe kutoka visiwani, huku utata mkubwa ukiwa kwenye kura ya Zakhia Meghji ambaye kwenye Kamati za Bunge la Katiba alishiriki kama mjumbe wa Bara lakini kwenye kura za kupitisha Katiba alishiriki kama mjumbe wa Zanzibar.

Alipotakiwa aeleze kama anaona kuna matumaini ya kupata Katika Mpya katika mazingira ambayo Taifa limegawanyika kimtazamo kuhusu mchakato wenyewe, Dk Kijo – Bisimba alisema mchakato huo una dosari nyingi, ikiwamo baadhi ya vifungu kuwekwa kama kiini macho ili kuwadanganya Watanzania.

“Sisi tangu mwanzo tulikuwa na mambo matatu ambayo tuliyafuatilia kwa karibu kwenye mchakato huo; haki za binadamu, utawala bora na maadili.

“Hatukuridhika na mchakato wenyewe pamoja na maudhui yake. Kwenye mchakato tulipinga suala la kuwashirikisha wanasiasa, tulitaka wanasiasa wawe ni moja ya tatu tu (ya Bunge lote) na wengine wawe theluthi mbili. Lakini tukapingwa. Hilo la kuwaongeza wanasiasa ndilo limechangia Bunge kukosa uhalali.”

Dk Kijo – Bisimba alibainisha kuwa idadi kubwa ya wanasiasa kwenye Bunge la Katiba ndiyo iliyoleta matatizo mengi katika mchakato wa mabadiliko ya Katiba, likiwamo tatizo la kura kupitisha Katiba Inayopendekezwa.
“Ili kuunusuru mchakato wa Katiba, tunapaswa kujitathmini, kinyume chake kutangazwa kupatikana kwa Katiba Mpya kunaweza kuwa mwanzo wa Watanzania kudai Katiba Mpya.”
Kuhusu makosa yaliyofanywa na Bunge la Katiba alisema, lilipaswa kutumia Rasimu ya Katika iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba, lakini kinyume chake likabadilisha maeneo mengi na kuweka kwenye Katiba Inayopendekezwa ambayo hayakutokana na maoni ya wananchi.
“Kuondoka kwa Ukawa bungeni kusingeleta shida kwenye mchakato wa Katiba kama waliobaki wangetenda haki. Lakini hawa sasa wakatumia fursa hiyo kubadilisha kanuni ili watengeneze Katiba wanayoona inafaa. Kuboresha siyo kuweka viraka. Kama ilivyo kwamba nikitaka kuboresha gauni langu ninapaswa kulishona na siyo kuweka vipande vya nguo nyingine,” alisema.
Alisema Katiba Inayopendekezwa pia ina kasoro ya kutambua haki za binadamu zilizopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba... “Haki za binadamu zimeandikwa kwa kalamu ya risasi kwenye Katiba hii. Sisi hatukuridhika na haki ya kuishi, haki ya afya na matumizi ya rasilimali. Lakini Bunge halikujali kwa sababu kwenye haki hizi hakukuwa na vipengele vya namna ya kuzitekeleza. Kwa mfano, kwenye haki ya kumiliki ardhi, Bunge liliongeza haki za wavuvi na wachimba madini. Sasa mvuvi na ardhi wapi na wapi? Hapa wanatudanganya na hiki ni kiini macho.” Asante kwa kutembelea blog hii na endelea kuwa nasi siku zote, kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz
Dk Kijo – Bisimba alieleza kuwa suala jingine ambalo taasisi hiyo imeona ni kasoro kwenye Katiba hiyo ni kuondoa kipengele cha mikataba kuridhiwa na Bunge na rais kupunguziwa madaraka ya uteuzi.
Alisema utaratibu uliowekwa na Tume ya Jaji Warioba kwamba kuundwe vyombo vya uteuzi, ulikuwa mzuri na ungesaidia kupunguza uwezekano wa mkuu huyo wa nchi, kuchagua watu kulingana na masilahi yake.
“Kama kutakuwa na chombo cha uteuzi, halafu majina yakaenda kwa rais na baadaye bungeni, utaona kwamba walau kuna udhibiti, lakini ilivyo kwamba rais ateue watu moja kwa moja ni tatizo,” alisema.
Kuhusu utawala, alisema Bunge limekosea kuondoa kipengele hicho kwenye Rasimu ya Katiba ya Tume ya Jaji Warioba kinachotaka mawaziri wasiwe wabunge, kwani hatua hiyo inawafanya washindwe kuwajibika serikalini. Pia Bunge limekosea kuendelea kumweka rais sehemu ya Bunge.
“Rasimu ya Warioba ilitaka Bunge liisimamie Serikali, lipitie mikataba na mamlaka ya Rais ya uteuzi yapungue. Lakini wakaondoa hayo yote kwa masilahi yao,” alisema.
Uzalendo
Dk Kijo – Bisimba aliitaja kasoro nyingine kwenye Katiba Inayopendezwa kuwa ni kuondolewa kwa tunu za Taifa kutoka kwa wananchi wa kawaida na kuzipeleka kwa viongozi.
“Tunu kama uzalendo, uwajibikaji na nyingine zimeondolewa na Bunge na kuzipeleka kuwa tunu za viongozi. Sasa utampata kiongozi mwenye tunu hizo kama hatokani na jamii inayozienzi?” alihoji.
Alisema Taifa lilipofikia, linahitaji kuwa na tunu ambazo zitakuwa msingi wa maadili, vinginevyo tatizo la mmomonyoko wa maadili litaendelea na kutishia mustakabali wa Taifa.
50 kwa 50
Akizungumzia uwiano wa jinsia wa 50 kwa 50, Dk Kijo – Bisimba alisema Katiba Inayopendekezwa imeondoa dhana hiyo kabisa.
“Ibara ya 134 (2) ya Rasimu Inayopendekezwa imeeleza kuwa idadi ya wabunge itakuwa kati ya 340 na 390 kwa kuzingatia uwiano wa jinsia. Sasa kuzingatia ni kuzingatia tu, kama utazingatia lakini hakuna mwanamke aliyejitokeza maana yake nini? Utasema tumezingatia lakini hali ndiyo hiyo,” alisema.
“Katiba hii ilipaswa kueleza kwamba katika kila jimbo kutakuwa na wagombea wanaume na wanawake watakaoshindana kuwania uongozi, vinginevyo Katiba hiyo imeturudisha nyuma, tena unaweza kusema afadhali ya Katiba ya mwaka 1977 kwa sababu ilisema kutakuwa na asilimia 30 ya uwakilishi wa wanawake bungeni.”
Hii si mara ya kwanza kwa Dk Kijo – Bisimba kutofautiana na mchakato mzima wa Katiba.
Katika hatua za awali, taasisi yake ilikuwa ikifanya kazi kubwa ya kuelimisha wananchi kuhusu Katiba chini ya kampeni yake ya Gogota na mara kadhaa alilaumu viongozi wa mikoa kwa kukwamisha juhudi zao za kuelimisha wananchi kuhusu haki zao kwenye nyaraka hiyo muhimu kwao na kuwahimisha kushiriki kikamilifu. Asante kwa kutembelea blog hii na endelea kuwa nasi siku zote, kuwa wa kwanza kupata habari zetu kwa ku-Like page yetu ya facebook kwa ku-click/ bofya neno Jambo Tz

Na Mwananchi

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...