Tuesday, January 13, 2015

"WALIOJITOKEZA KUWANIA URAIS CCM HAWANA SIFA" KINGUNGE


Mwanasiasa mkongwe nchini Mzee Kingunge Ngombare Mwiru akizungumza na wanahabari. Picha na Maktaba 

Harakati za kuwania urais ndani ya CCM zimeingia katika hatua mpya baada ya mwanasiasa mkongwe, Kingunge Ngombale - Mwiru kuibuka na kudai kuwa wote waliojitokeza kuwania nafasi hiyo hawana sifa kwa kuwa wanatumia fedha kutaka kuingia Ikulu.
Kauli ya mwanasiasa huyo ambayo imekuja siku moja kabla ya Kamati Kuu ya CCM kukutana leo mjini Unguja na moja ya ajenda ikitajwa kuwa suala la maadili, inaweza kuwa mwiba mchungu kwa wanasiasa hao ambao wanaongezeka kila kukicha.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Kingunge alisema: “Kuna suala la kukosa uadilifu, kuna suala la matumizi ya pesa na nikwambie ukweli, hao wanaotangaza urais wote wanatumia pesa, wanatumia faulo mbalimbali na wananchi wanajua.” Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.
Kwa miezi kadhaa sasa, baadhi ya makada wa CCM wamekuwa wakitajwa kufanya harakati kichinichini na wengine kushiriki shughuli za wazi zinazoashiria kuwa wanataka kuwania nafasi hiyo ya juu. Hadi sasa makada wanne tayari wameweka wazi nia yao hiyo.
Hivi karibuni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba kwa nyakati tofauti walitoa kauli zinazowashutumu makada wengine wa chama hicho kwa matumizi makubwa ya fedha katika kushawishi uungwaji mkono.
Hata hivyo, kauli za wanasiasa hao zimedaiwa kuwa ni fitina za kisiasa kwa kuwa wagombea wote wanatoa fedha, bali wanazidiana viwango tu.
Mbali na Makamba na Membe, wanaCCM wengine waliotangaza au kutajwa kuwania urais ni Mbunge wa Nzega, Dk Khamis Kigwangalla, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Wengine ni mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Stephen Wasira na aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja.
Kauli ya Kingunge aliyoitoa kupitia Televisheni ya ITV, imekuja wakati wanasiasa sita miongoni mwa hao wanaotajwa wakikaribia kumaliza miezi 12 ya uangalizi kutokana na onyo kali dhidi yao lililotolewa na Kamati Kuu ya CCM Februari 18, mwaka jana baada ya kuwatia hatiani kwa makosa ya “kuanza kampeni mapema na kufanya mambo ambayo ni kinyume na maadili ya chama na ya jamii.”
Wanaotumikia adhabu hiyo ni Lowassa, Sumaye, Njeleja, Makamba, Wasira na Membe.
Akisisitiza hoja yake hiyo bila kutaja majina, Kingunge alisema makada hao wamekuwa wakitumia fedha nyingi kujitangaza na kutengeneza ushawishi wa kukubalika kwa wananchi jambo ambalo ni kinyume na maadili ya uongozi.
Kingunge alisema mwanasiasa yeyote anayehitaji uongozi hapaswi kutumia fedha kushawishi wananchi wamchague. Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.
“Kiukweli tukiangalia wote wanaojitangaza hakuna msafi hata mmoja... hatuwezi kuchagua rais kama vile tunachagua wachezaji wa mpira, haiwezekani. Tunataka kupata mgombea wa urais ambaye atakuwa na uwezo wa kushughulikia kwa vitendo kero na umaskini wa Watanzania,” alisema Kingunge.
Alisema badala ya viongozi kutumia muda mrefu kumtafuta mchawi, ni vyema wakatazama namna ya kushughulikia suala la maadili kwa sababu kati yao hakuna msafi hata mmoja.
Kuhusu watu wengi kujitokeza kutaka urais, Kingunge alisema: “Kujitokeza kugombea urais siyo dhambi, ingawa watu wanashangaa kidogo kwamba kila mtu anaibuka tu anataka urais, kidogo inaleta kasoro lakini siyo kitu, wanataka kutumia haki zao.”
Mkongwe huyo wa siasa alisema wananchi ndiyo wanaowajua wagombea hao na sifa zao, hivyo wakumbuke kuwa anayechaguliwa ni rais na siyo mchezaji wa mpira.
“Mnachagua rais ambaye ataweza kuwaunganisha kama Taifa, ataweza kuwatumikia kwa vitendo siyo kujitumikia wenyewe, pia ataweza kutatua matatizo yanayowakabili wananchi,” alisema.
Aliongeza kwamba kwa kuwa tatizo kubwa la wananchi ni umaskini, wananchi watazame mtu atakayeweza kuondoa hali hiyo.
Akizungumzia kuhusu namna viongozi wa Afrika wanavyoyatumia madaraka yao, Kingunge alisema wamepiga hatua kubwa lakini bado haitoshi kwa kuwa wanakosa namna chanya ya kutumia madaraka ambayo Afrika iliyapigania kutoka kwa wakoloni.
“Tumeupigania uhuru ili tuendeshe nchi yetu wenyewe, turudishe ile thamani yetu kama watu. Sasa madaraka tumepata, lakini tunayatumiaje?” alihoji.
Kuhusu Mapinduzi
Kuhusu Mapinduzi ya Zanzibar yaliyotimiza miaka 51 jana, Kingunge alisema yamekuwa na faida kubwa kwa Wazanzibari.
Alisema Mapinduzi hayo ndiyo msingi wa Muungano ambao umeleta mafanikio makubwa kwa pande zote licha ya changamoto zinazoibuliwa.
“Haikuwa na budi kufanya mapinduzi kwa kuunda kamati ya wapiganaji 14 ambao waliongoza kazi hiyo baada ya kuona mfumo uliokuwa unatumiwa na Serikali ya Sultan unawakandamiza wazawa. Baada ya mapinduzi hayo kufanikiwa, ardhi iliyokuwa inamilikiwa na kundi moja la Waarabu ikagawanywa kwa kila Mzanzibari akapata ekari tatu, pamoja na hali hiyo elimu ilitangazwa kutolewa bure.”  Tangaza biashara yako hapa kwa bei nafuu zaidi, pia usisahau ku-Like Ukurasa Wetu Wa Facebook Kwa Kubofya/ Click Neno Jambo Tz.

Na Mwananchi 

No comments:

Pro

PropellerAds

LinkWithin

Soma na Hizi Pia Plugin for WordPress, Blogger...