Mabingwa wa soka la Tanzania bara Yanga SC wameanza vibaya kampeni
zao za kuwania kombe la Shirikisho Afrika baada ya kupoteza mchezo wao
wa kwanza kwa bao 1-0 dhidi ya MO Bejaia ukiwa ni chezo wa Kundi A.
Yassin Sahli alifunga bao pekee kwenye mchezo huo na kuipa pointi
tatu MO Bejaia iliyokuwa ikicheza kwenye uwanja wake wa nyumbani Stade
de I’Unite Maghrebine mjini Bejaia, Algeria.
Matokeo hayo yanaiacha Yanga katika nafasi ya tatu huku TP Mazembe
wakiwa ndiyo vinara wa Kundi baada ya kushinda mchezo wao kwa magoli 3-0
dhidi ya Medeama ambayo inaburuza mkia.
Mazembe na MO Bejaia zinapointi sawa (pointi tatu) lakini TP Mazembe
anaongoza kundi kwa tofauti ya magoli wakati Yanga na Medeama zikiwa
hazina pointi lakini Yanga inakaa nafasi ya tatu kwa tofauti ya magoli.
Medeama imefungwa magoli matatu wakati Yanga wameruhusu bao moja pekee.
Mchezo ujao wa Yanga utakuwa nyumbani (Dar es Salaam) June 28 itakapowaalika TP Mazembe kwenye uwanja wa taifa.